لقمان
Luqman • 34 ayahs • Meccan
بِسْمِ ٱللَّهِ ٱلرَّحْمَٰنِ ٱلرَّحِيمِ
1Alif Laam Miim.[1]
2Hizi ni Aya za Kitabu chenye hekima.
3Kuwa ni uongofu na rehema kwa wafanyao wema.
4Wale wanaoshika Swala, na wanatoa Zaka, nao wana yakini na Akhera.
5Hao ndio walio kwenye uongofu utokao kwa Mola wao Mlezi, na hao ndio waliofaulu.
6Na miongoni mwa watu wapo wanaonunua maneno ya upuuzi, ili wawapoteze watu mbali na njia ya Mwenyezi Mungu pasipo kujua, na wanaichukulia ni masihara. Hao watapata adhabu ya kuwafedhehesha.
7Na mtu kama huyo anaposomewa Aya zetu, huzipa mgongo kwa kujivuna, kana kwamba hakuzisikia, au masikioni mwake mna uziwi. Basi mbashirie kuwa atapata adhabu chungu.
8Hakika walioamini na wakatenda mema watakuwa na Bustani za neema.
9Watadumu humo, ni ahadi ya Mwenyezi Mungu ya kweli. Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hekima.
10Ameziumba mbingu bila ya nguzo mnazoziona, na ameweka katika ardhi milima ili ardhi isiwayumbishe, na ametawanya humo kila namna ya wanyama, na tumeteremsha maji kutoka mbinguni, na tukaotesha katika ardhi mimea mizuri ya kila namna.
11Huu ni uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Basi nionyesheni wameumba nini hao wasiokuwa Yeye! Lakini madhalimu wamo katika upotovu ulio dhahiri.
12Na tulimpa Luqman hekima, tukamwambia; "Mshukuru Mwenyezi Mungu." Na mwenye kushukuru, basi hakika anashukuru kwa manufaa ya nafsi yake. Na aliyekufuru, basi Mwenyezi Mungu ni Mkwasi, Msifiwa.
13Na Luqman alipomwambia mwanawe kwa kumpa mawaidha, "Ewe mwanangu, usimshirikishe Mwenyezi Mungu. Kwani, hakika ushirikina bila ya shaka ni dhuluma iliyo kubwa."
14Na tumemuusia mtu kwa wazazi wake wawili. Mama yake ameichukua mimba yake kwa udhaifu juu ya udhaifu, na kumwachisha ziwa baada ya miaka miwili. Tumemuusia, "Nishukuru Mimi na wazazi wako. Ni kwangu Mimi ndiyo marejeo yenu."
15Na pindi wakikushikilia kunishirikisha na ambayo huna elimu nayo, basi usiwatii. Lakini kaa nao kwa wema duniani, nawe ishike njia ya anayeelekea kwangu. Kisha marejeo yenu ni kwangu Mimi, na Mimi nitawaambia yale mliyokuwa mkiyatenda.
16"Ewe mwanangu, kikiwapo kitu cha uzito wa chembe ya khardali kikawa ndani ya jabali au ndani ya mbingu au ndani ya ardhi, basi Mwenyezi Mungu atakileta. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa yaliyofichika, Mwenye habari za yote.
17Ewe mwanangu, shika Swala, na amrisha mema, na kataza maovu, na subiri kwa yanayokupata. Hayo ni katika mambo ya kuazimiwa.
18Wala usiwabeuwe watu, wala usitembee katika nchi kwa maringo. Hakika Mwenyezi Mungu hampendi kila anayejivuna na kujifakhirisha.
19Na kuwa wa hali ya katikati katika kutembea kwako, na teremsha chini sauti yako. Hakika katika sauti mbaya kuliko zote ni sauti ya punda.
20Kwani hamwoni ya kwamba Mwenyezi Mungu amevifanya vikutumikieni vilivyomo mbinguni na kwenye ardhi, na akakujalizieni neema zake, za dhahiri na za siri? Na miongoni mwa watu wapo wanaobishana juu ya Mwenyezi Mungu pasipo elimu, wala uongofu, wala Kitabu chenye nuru.
21Na wanapoambiwa, "Fuateni aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu," husema: "Bali tunafuata tuliyowakuta nayo baba zetu". Je, hata kama Shetani anawaita kwenye adhabu ya Moto wenye mwako mkali?
22Na mwenye kuuelekeza uso wake kwa Mwenyezi Mungu, naye akawa anafanya wema, basi huyo hakika amekwisha kamata fundo lililo madhubuti. Na mwisho wa mambo yote ni kwa Mwenyezi Mungu.
23Na anayekufuru, isikuhuzunishe kufuru yake. Kwetu ndiyo marudio yao, na hapo tutawaambia waliyoyatenda. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa yaliyomo vifuani.
24Tunawastarehesha kwa uchache, kisha tutawasukuma kwenye adhabu ngumu.
25Na ukiwauliza nani aliyeziumba mbingu na ardhi? Bila shaka watasema, Mwenyezi Mungu. Wewe sema Alhamdulillahi! Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu. Lakini wengi wao hawajui.
26Ni vya Mwenyezi Mungu vyote vilivyomo mbinguni na katika ardhi. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mkwasi, Mwenye kusifiwa.
27Na lau kuwa miti yote iliyomo duniani ikawa ni kalamu, na bahari ikawa wino, na ikaongezewa juu yake bahari nyengine saba, maneno ya Mwenyezi Mungu yasingelikwisha. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.
28Hakukuwa kuumbwa kwenu, wala kufufuliwa kwenu ila ni kama nafsi moja tu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.
29Kwani huoni kwamba Mwenyezi Mungu huuingiza usiku katika mchana, na huuingiza mchana katika usiku, na amedhalilisha jua na mwezi? Vyote hivyo vinakwenda mpaka wakati uliowekwa. Na Mwenyezi Mungu anazo habari za mnayoyatenda.
30Hivi ni kwa sababu, Mwenyezi Mungu ndiye wa kweli, na hakika wanachokiomba ni cha uongo. Na kwamba hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mtukufu na ndiye Mkubwa.
31Kwani huoni kwamba merikebu hupita baharini kwa neema za Mwenyezi Mungu, ili kuwaonyesha baadhi ya Ishara zake? Hakika katika haya zipo Ishara kwa kila mwenye kusubiri na mwenye kushukuru.
32Na wimbi linapowafunika kama wingu, wao humwomba Mwenyezi Mungu kwa kumsafia dini. Lakini anapowaokoa wakafika nchi kavu, wapo baadhi yao huwa wa kati na kati. Wala hazikanushi Ishara zetu ila aliyekhaini kafiri mkubwa.
33Enyi watu, mcheni Mola wenu Mlezi, na iogopeni siku ambayo mzazi hatamfaa mwana, wala mwana hatamfaa mzazi kwa lolote. Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya kweli. Basi yasiwadanganyeni maisha ya dunia, wala asiwadanganyeni na Mwenyezi Mungu yule mdanganyifu.
34Hakika kuijua Saa ya Kiyama kuko kwa Mwenyezi Mungu. Na Yeye ndiye anayeiteremsha mvua. Na anavijua vilivyo ndani ya matumbo ya uzazi. Na haijui nafsi yoyote itachuma nini kesho. Wala nafsi yoyote haijui itafia nchi gani. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kujua, Mwenye habari.