الصافات
Those Ranged in Ranks • 182 ayahs • Meccan
بِسْمِ ٱللَّهِ ٱلرَّحْمَٰنِ ٱلرَّحِيمِ
1Ninaapa kwa wanaojipanga kwa safu.
2Na kwa wenye kukataza mabaya.
3Na kwa wenye kusoma Ukumbusho.
4Hakika Mungu wenu bila ya shaka ni Mmoja.
5Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, na yaliyomo kati yake, na ni Mola Mlezi wa mashariki zote.
6Hakika Sisi tumeipamba mbingu ya karibu kwa pambo la nyota.
7Na kulinda na kila shetani muasi.
8Wasiweze kuwasikiliza viumbe watukufu. Na wanafukuzwa huko kila upande.
9Wakifurushwa. Na wanayo adhabu ya kudumu.
10Isipokuwa anayenyakua kitu kidogo, na mara humfwatia kimondo kinachong'ara.
11Hebu waulize: Je! Wao ni wenye umbo gumu zaidi au hao wengine tuliowaumba. Hakika Sisi tuliwaumba wao kwa udongo unaonata.
12Bali unastaajabu, na wao wanafanya masihara.
13Na wanapokumbushwa, hawakumbuki.
14Na wanapoona Ishara, wanafanya masihara.
15Na husema: Haya si chochote isipokuwa ni uchawi tu ulio dhahiri.
16Ati tukishakufa na tukawa udongo na mifupa ndio kweli tutafufuliwa?
17Hata baba zetu wa zamani?
18Sema: Naam! Hali nanyi ni madhalili.
19Huko utapigwa ukelele mmoja tu! Na hapo ndipo wataona!
20Watasema: Ole wetu! Hii ndiyo Siku ya Malipo.
21Hii ndiyo Siku ya Hukumu mliyokuwa mkiikadhibisha.
22Wakusanyeni wale waliodhulumu, na wote walio mfano wao, na hao ambao wao walikuwa wakiwaabudu.
23Badala ya Mwenyezi Mungu. Waongozeni njia ya Jahannamu!
24Na wasimamisheni. Hakika hao wataulizwa:
25Mna nini? Mbona hamsaidiani?
26Bali hii leo, watasalimu amri.
27Wataelekeana wao kwa wao kuulizana.
28Watasema: Kwa hakika nyinyi mlikuwa mkitujia upande wa kulia.
29Watasema (wakubwa): Bali nyinyi wenyewe hamkuwa Waumini.
30Sisi hatukuwa na mamlaka juu yenu, bali nyinyi wenyewe mlikuwa wapotovu.
31Basi hukumu ya Mola wetu Mlezi imekwisha tuthibitikia. Hakika bila ya shaka tutaonja tu adhabu.
32Tulikupotezeni kwa sababu sisi wenyewe tulikuwa wapotovu.
33Basi wao kwa hakika siku hiyo watashirikiana katika adhabu pamoja.
34Hivyo ndivyo tutakavyowafanyia wahalifu.
35Wao walipokuwa wakiambiwa, "La ilaha illallaahu (Hapana mungu ila Mwenyezi Mungu tu)", wanajivuna.
36Na wakisema: Hivyo sisi tuiache miungu yetu kwa ajili ya huyu mtunga mashairi mwendawazimu?
37Bali huyu amekuja kwa haki, na amewasadikisha Mitume.
38Hakika nyinyi bila ya shaka mtaionja adhabu chungu.
39Wala hamlipwi isipokuwa hayo mliyokuwa mkiyafanya.
40Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu walioteuliwa.
41Hao ndio watakaopata riziki maalumu.
42Matunda, nao wataheshimiwa.
43Katika Bustani za neema.
44Wako juu ya viti mfano wa kitanda wameelekeana.
45Wanazungushiwa kikombe chenye kinywaji cha chemchemi.
46Kinywaji cheupe, kitamu kwa wanywao.
47Hakina madhara, wala hakiwaleweshi.
48Na watakuwa nao wanawake wenye macho ya staha, mazuri.
49Hao wanawake kama mayai yaliyohifadhika.
50Basi wakaelekeana kuulizana wenyewe kwa wenyewe.
51Aseme msemaji mmoja miongoni mwao: Hakika mimi nilikuwa na rafiki.
52Aliyekuwa akiniambia: Hivyo wewe ni katika wanaosadiki.
53Ati tukishakufa tukawa udongo na mafupa, ndiyo tutalipwa na kufanyiwa hesabu?
54Atasema: Je, nyie mnawaona?
55Basi atachungulia amwone katikati ya Jahannamu.
56Atasema: Wallahi! (Naapa kwa jina la Mwenyezi Mungu) Ulikaribia sana kunipoteza.
57Na lau kuwa si neema ya Mola wangu Mlezi, bila ya shaka ningelikuwa miongoni mwa waliohudhurishwa.
58Je, sisi hatutakufa?
59Isipokuwa kifo chetu cha kwanza? Wala sisi hatutaadhibiwa.
60Hakika huku bila ya shaka ndiko kufuzu kukubwa.
61Kwa mfano wa haya na watende watendao.
62Je, kukaribishwa hivi si ndiyo bora, au mti wa Zaqqum?
63Hakika Sisi tumeufanya huo kuwa ni mateso kwa waliodhulumu.
64Hakika huo ni mti unaotoka katikati ya Jahannamu.
65Mashada ya matunda yake kama kwamba ni vichwa vya mashetani.
66Basi hakika bila ya shaka hao watayala hayo, na wajaze matumbo kwayo.
67Kisha juu yake wanyweshwe mchanganyo wa maji ya moto yaliyochemka.
68Kisha hakika marejeo yao bila ya shaka yatakuwa Jahimu.
69Hakika waliwakuta baba zao wamepotea.
70Na wao wakafanya haraka kufuata nyayo zao.
71Na bila ya shaka walikwisha potea kabla yao wengi wa watu wa zamani.
72Na Sisi hakika tuliwapelekea waonyaji.
73Basi hebu angalia ulikuwaje mwisho wa walioonywa.
74Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliosafishwa.
75Na hakika Nuhu alituita, na Sisi ni bora wa waitikiaji.
76Na tulimwokoa yeye na ahali zake kutokana na msiba mkubwa.
77Na tuliwajaalia dhuria zake ndio wenye kubakia.
78Na tukamwachia (sifa njema) kwa waliokuja baadaye.
79Iwe salama kwa Nuhu ulimwenguni kote!
80Kwa hakika hivi ndivyo tunavyowalipa wanaofanya mema.
81Hakika yeye ni katika waja wetu walioamini.
82Kisha tukawazamisha wale wengine.
83Na hakika Ibrahim alikuwa katika kundi lake.
84Alipomjia Mola wake Mlezi kwa moyo mzima.
85Alimwambia baba yake na watu wake: Mnaabudu nini?
86Kwa kuzua tu mnataka miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu?
87Mnamdhania nini Mola Mlezi wa walimwengu wote?"
88Kisha akapiga jicho kutazama nyota.
89Akasema: Hakika mimi ni mgonjwa!
90Nao wakamwacha, wakampa kisogo.
91Basi akaiendea miungu yao kwa siri, akaiambia: Mbona hamli?
92Mna nini hata hamsemi?
93Kisha akaigeukia kuipiga kwa mkono wa kulia.
94Basi wakamjia upesi upesi.
95Akasema: Hivyo mnaviabudu vitu mnavyovichonga wenyewe?
96Na hali Mwenyezi Mungu ndiye aliyekuumbeni nyinyi na hivyo mnavyovifanya!
97Wakasema: Mjengeeni jengo, na kisha mtupeni motoni humo!
98Basi walitaka kumfanyia vitimbi, lakini tukawafanya wao ndio wa chini zaidi.
99Na akasema: Hakika mimi nahama, nakwenda kwa Mola wangu Mlezi; Yeye ataniongoa.
100Ewe Mola wangu Mlezi! Nitunukie aliye miongoni mwa watenda mema.
101Basi tukambashiria mwana aliye mpole.
102Basi alipofika makamo ya kwenda na kurudi pamoja naye, alimwambia: Ewe mwanangu! Hakika mimi nimeona usingizini kuwa ninakuchinja. Basi angalia wewe, waonaje? Akasema: Ewe baba yangu! Tenda unavyoamrishwa, utanikuta mimi, Insha Allah (Mwenyezi Mungu akipenda), katika wanaosubiri.
103Basi wote wawili walipojisalimisha, na akamlaza juu ya kipaji.
104Tulimwita: Ewe Ibrahim!
105Umekwisha itimiliza ndoto. Hakika hivi ndivyo tunavyowalipa wanaotenda mema.
106Hakika haya ni majaribio yaliyo dhahiri.
107Basi tukamtolea fidia kwa dhabihu mtukufu.
108Na tukamwachia (sifa njema) kwa watu waliokuja baadaye.
109Iwe salama kwa Ibrahim!
110Hivi ndivyo tunavyowalipa wanaofanya mema.
111Hakika yeye ni katika waja wetu walioamini.
112Na tukambashiria kuzaliwa Is-haqa, naye ni Nabii miongoni mwa watu wema.
113Na tukambarikia yeye na Is-haqa. Na miongoni mwa dhuria zao walitokea wema na wenye kudhulumu nafsi zao waziwazi.
114Na kwa hakika tuliwafanyia hisani Musa na Haruni.
115Na tukawaokoa wao na watu wao kutokana na dhiki kubwa.
116Na tukawanusuru; na wakawa wao ndio wenye kushinda.
117Na tukawapa wawili hao Kitabu kinachobainisha.
118Na tukawaongoa kwenye njia iliyonyooka.
119Na tukawaachia (sifa njema) katika watu waliokuja baadaye.
120Iwe salama kwa Musa na Haruni!
121Hakika hivyo ndivyo tunavyowalipa walio wema.
122Hakika wawili hao ni katika waja wetu walioamini.
123Na hakika Ilyas bila ya shaka alikuwa miongoni mwa Mitume.
124Alipowaambia watu wake: Hamumchi Mungu?
125Mnamwomba Baa'li na mnamwacha Mbora wa waumbaji.
126Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wenu na Mola Mlezi wa baba zenu wa zamani?
127Wakamkadhibisha. Basi kwa hakika watahudhurishwa.
128Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliosafishwa.
129Na tumemwachia (sifa nzuri) kwa waliokuja baadaye.
130Iwe salama kwa Ilyas.
131Hakika hivyo ndivyo tunavyowalipa walio wema.
132Hakika yeye ni katika waja wetu walioamini.
133Na hakika Lut'i bila ya shaka ni miongoni mwa Mitume.
134Tulipomwokoa yeye na ahali zake wote.
135Isipokuwa mwanamke mkongwe katika wale waliobakia nyuma.
136Kisha tukawaangamiza wale wengineo.
137Na hakika nyinyi mnawapitia wakati wa asubuhi.
138Na usiku. Basi je, hamyatii akilini?
139Na hakika Yunus alikuwa miongoni mwa Mitume.
140Alipokimbia akenda katika jahazi lililosheheni.
141Akaingia katika kupigiwa kura, na akawa katika walioshindwa.
142Samaki akammeza hali ya kuwa ni mwenye kulaumiwa.
143Na ingelikuwa hakuwa katika wanaomtakasa Mwenyezi Mungu.
144Bila ya shaka angelikaa ndani yake mpaka siku ya kufufuliwa.
145Lakini tulimtupa ufukweni patupu, hali yu mgonjwa.
146Na tukauotesha juu yake mmea wa aina ya mung'unye.
147Na tulimtuma kwa watu laki moja au zaidi.
148Basi wakaamini, na tukawastarehesha kwa muda.
149Basi waulize: Ati Mola wako Mlezi ndiye mwenye watoto wa kike, na wao wanao watoto wa kiume?
150Au tumewaumba Malaika kuwa ni wanawake, na wao wakashuhudia?
151Tazama, hakika ni kwa uzushi wao ndio wanasema.
152Mwenyezi Mungu amezaa! Ama hakika bila ya shaka hao ni waongo!
153Ati amehiari watoto wa kike kuliko wanaume?
154Mna nini? Mnahukumu vipi nyinyi?
155Hamkumbuki?
156Au mnayo hoja iliyo wazi?
157Basi leteni Kitabu chenu kama nyinyi ni wakweli.
158Na wameweka mahusiano ya nasaba baina yake na majini; na majini wamekwishajua bila ya shaka kuwa wao watahudhurishwa.
159Ametakasika Mwenyezi Mungu mbali na hayo wanayomsingizia.
160Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliosafishwa.
161Basi hakika nyinyi na mnaowaabudu.
162Hamwezi kuwapoteza.
163Isipokuwa yule atakayeingia Motoni.
164Na hapana katika sisi ila anapo mahali pake maalumu.
165Na hakika bila ya shaka sisi ndio wajipangao safu.
166Na hakika sisi ndio wenye kutakasa.
167Na walikuwapo waliokuwa wakisema.
168Tungelikuwa na Ukumbusho kama wa watu wa zamani.
169Bila ya shaka tungelikuwa ni waja wa Mwenyezi Mungu wenye kumkusudia Yeye tu.
170Lakini waliukufuru. Basi watakuja jua.
171Na bila ya shaka neno letu lilikwisha tangulia kwa waja wetu waliotumwa.
172Ya kuwa wao bila ya shaka ndio watakaonusuriwa.
173Na kwamba jeshi letu ndilo litakaloshinda.
174Basi waachilie mbali kwa muda.
175Na watazame, nao wataona.
176Je, wanaiharakishia adhabu yetu?
177Basi itakaposhuka uwanjani kwao, itakuwa asubuhi mbaya kwa walioonywa.
178Na waache kwa muda.
179Na tazama, na wao wataona.
180Ametakasika Mola wako Mlezi Mwenye utukufu mbali na yale wanayomzulia.
181Na Salamu juu ya Mitume.
182Na sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote.