آل عمران
Family of Imran • 200 ayahs • Medinan
بِسْمِ ٱللَّهِ ٱلرَّحْمَٰنِ ٱلرَّحِيمِ
1Alif Laam Miim.[1]
2Mwenyezi Mungu, hakuna mungu isipokuwa Yeye. Aliye hai, Msimamizi wa yote milele.
3Amekiteremsha Kitabu juu yako kwa haki, kinachosadikisha yaliyokuwa kabla yake. Na aliteremsha Taurati na Injili.
4Kabla yake, viwe uongofu kwa watu. Na akateremsha Furqani (Upambanuo). Hakika, wale waliozikufuru Ishara za Mwenyezi Mungu wana adhabu kali. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye kulipiza.
5Hakika, Mwenyezi Mungu hakifichikani chochote kwake, katika dunia wala katika mbingu.
6Yeye ndiye anayewaunda ndani ya matumbo ya uzazi kwa namna apendavyo. Hakuna mungu isipokuwa Yeye, Mwenye nguvu, Mwenye hekima.
7Yeye ndiye aliyeteremsha juu yako Kitabu hiki. Ndani yake zimo Aya muhkam (zenye maana wazi). Hizo ndizo msingi wa Kitabu hiki. Na zimo nyingine Mutashabihat (zenye maana zisizo wazi). Ama wale ambao katika nyoyo zao umo upotovu, wao wanafuata zile zenye maana zisizo wazi kwa kutafuta fitina, na kutafuta kupotoa maana yake. Na wala hapana ajuaye maana yake isipokuwa Mwenyezi Mungu. Na wale waliokita katika elimu husema: Sisi tumeziamini, zote zimetoka kwa Mola wetu Mlezi. Lakini hawakumbuki (hayo) isipokuwa wenye akili ya hali ya juu.
8(Na wao husema) Mola wetu Mlezi! Usizipotoe nyoyo zetu baada ya kutuongoa, na tutunuku rehema itokayo kwako. Hakika, Wewe ndiye Mwenye kutunuku mno.
9Mola wetu Mlezi! Hakika, Wewe ndiye utakayewakusanya watu kwa Siku isiyo na shaka ndani yake. Hakika, Mwenyezi Mungu havunji miadi yake.
10Kwa hakika, wale waliokufuru, hazitawafaa kitu mali zao wala watoto wao kutokana na Mwenyezi Mungu. Na hao ndio kuni za Moto.
11Kama ada ya watu wa Firauni na wale waliokuwa kabla yao. Walikadhibisha Ishara zetu, basi Mwenyezi Mungu akawachukua kwa dhambi zao; na Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.
12Waambie wale waliokufuru: Karibuni mtashindwa na mtakusanywa mtiwe kwenye Jahannam; napo ndipo pahali paovu zaidi pa mapumziko.
13Hakika, mlikuwa na Ishara katika yale makundi mawili yalipokutana (katika vita). Kundi moja likipigana katika Njia ya Mwenyezi Mungu, nalo lingine kafiri likiwaona zaidi kuliko wao mara mbili, kwa kuona kwa macho. Na Mwenyezi Mungu humuunga mkono amtakaye kwa nusura yake. Hakika, katika hayo kuna mazingatio kwa wenye macho yaliyo sawa.
14Watu wamepambiwa kupenda matamanio ya wanawake, na wana, na mirundo mingi ya dhahabu na fedha, na farasi wazuri zaidi, na mifugo, na mashamba. Hayo ni starehe ya maisha ya duniani, na Mwenyezi Mungu ana marejeo mazuri.
15Sema: Je, niwaambie yaliyo bora kuliko hayo? Kwa waliomcha Mungu kwa Mola wao Mlezi ziko Bustani zipitazo mito chini yake. Watadumu humo, na wake waliotakaswa, na radhi kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuwaona vyema waja wake.
16Wale wanaosema: Mola wetu Mlezi! Hakika, sisi tumeamini. Basi tusamehe dhambi zetu, na tuepushe kutokana na adhabu ya Moto.
17Wanaovumilia, na wakweli, na wanyenyekevu, na watoao, na wanao omba msamaha katika masaa ya mwisho ya usiku.
18Mwenyezi Mungu alishuhudia kuwa hakika hakuna mungu isipokuwa Yeye, na pia (walishuhudia) Malaika, na wenye elimu akisimamisha uadilifu. Hakuna mungu isipokuwa Yeye Mwenye nguvu, Mwenye hekima.
19Hakika, Dini kwa Mwenyezi Mungu ni Uislamu. Na hawakuhitilafiana wale waliopewa Kitabu isipokuwa baada ya kujiwa na elimu, kwa sababu ya uhasidi uliokuwa baina yao. Na mwenye kuzikufuru Ishara za Mwenyezi Mungu, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhesabu.
20Na wakikuhoji, basi sema: Mimi nimeusalimisha uso wangu kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na vile vile walionifuata. Na waambie wale waliopewa Kitabu na wale wasiojua kusoma: "Je, mmesilimu?" Wakisilimu, basi hakika wameongoka. Na wakikengeuka, basi juu yako ni kufikisha ujumbe tu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuwaona vyema waja wake.
21Hakika, wale wanaozikufuru Ishara za Mwenyezi Mungu, na wakawaua Manabii bila ya haki, na wakawaua wale wanaoamrisha haki katika watu, basi wabashirie adhabu kali.
22Hao ndio ambao vitendo vyao viliharibika duniani na Akhera. Nao hawana wowote wa kuwanusuru.
23Je, huwaoni wale waliopewa fungu katika Kitabu? Wanaitwa kukiendea Kitabu cha Mwenyezi Mungu ili kihukumu baina yao; kisha kundi miongoni mwao wanageuka huku wamepeana mgongo.
24Hayo ni kwa sababu walisema: "Hautatugusa Moto isipokuwa kwa siku chache tu." Na yakawadanganya katika dini yao yale ambayo wenyewe walikuwa wakiyazua.
25Basi itakuwaje tutakapowakusanya kwa ajili ya Siku ambayo hakuna shaka nayo? Na kila nafsi italipwa ilichochuma, nao hawatadhulumiwa.
26Sema: Ewe Mwenyezi Mungu uliye Mmiliki wa ufalme wote! Wewe humpa ufalme umtakaye, na humwondolea ufalme umtakaye. Na humtukuza umtakaye, na humdhalilisha umtakaye. Heri yote iko mkononi mwako. Hakika, Wewe ni Muweza wa kila kitu.
27Wewe huuingiza usiku katika mchana, na huuingiza mchana katika usiku. Na humtoa hai kutokana na maiti, na humtoa maiti kutokana na aliye hai. Na unamruzuku umtakaye bila ya hesabu.
28Waumini wasiwafanye makafiri kuwa marafiki wa kuwasaidia badala ya Waumini. Na mwenye kufanya hilo, basi hatakuwa na chochote mbele ya Mwenyezi Mungu. Isipokuwa ikiwa kwa ajili ya kujilinda na shari zao. Na Mwenyezi Mungu anawahadharisha naye mwenyewe. Na marejeo ni kwa Mwenyezi Mungu.
29Sema: Mkificha yaliyo vifuani mwenu au mkiyaweka wazi, Mwenyezi Mungu anayajua. Na anayajua yaliyo katika mbingu na yaliyo katika dunia. Na Mwenyezi Mungu ni Muweza mno wa kila kitu.
30Siku ambayo kila nafsi itakuta yale iliyofanya katika mema yamehudhurishwa, na pia yale iliyofanya katika ubaya. Itapenda lau baina ya hayo (mabaya) na yeye ungekuwepo umbali mrefu. Na Mwenyezi Mungu anawatahadharisha na yeye mwenyewe. Na Mwenyezi Mungu ni Mpole kwa waja wake.
31Sema: Ikiwa nyinyi mnampenda Mwenyezi Mungu, basi nifuateni mimi, Mwenyezi Mungu atawapenda na atawafutia dhambi zenu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kufuta dhambi, Mwenye kurehemu.
32Sema: 'Mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume.' Na wakigeuka, basi hakika Mwenyezi Mungu hawapendi makafiri.
33Hakika, Mwenyezi Mungu alimteua Adam, na Nuhu, na ukoo wa Ibrahim, na ukoo wa Imran juu ya walimwengu wote.
34Ni dhuria wao kwa wao. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.
35Aliposema mke wa Imran: Mola wangu Mlezi! Hakika mimi, nimekuwekea nadhiri kilicho katika tumbo langu la uzazi awe mtumishi wako, basi nikubalie. Hakika, Wewe ndiye Mwenye kusikia, Mwenye kujua.
36Basi alipomzaa, akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika mimi, nimemzaa wa kike - na Mwenyezi Mungu anajua sana aliyemzaa. Na wa kiume si sawa na wa kike. Na mimi kwa hakika nimemwita Mariam. Nami kwa hakika ninamkinga kwako, yeye na dhuria yake kutokana na Shetani aliyelaaniwa.
37Basi Mola wake Mlezi akampokea kwa mapokeo mema na akamkuza makuzo mema, na akamfanya Zakariya awe mlezi wake. Kila mara Zakariya alipoingia chumbani kwake, alimkuta na vyakula. Basi alisema: Ewe Mariam! Unavipata wapi hivi? Naye akasema: Hivi vinatoka kwa Mwenyezi Mungu. Hakika, Mwenyezi Mungu humruzuku amtakaye bila ya hesabu.
38Pale pale Zakariya akamwomba Mola wake Mlezi, akasema: Mola wangu Mlezi! Nitunuku kutoka kwako dhuria njema. Hakika, Wewe ndiye unayesikia maombi.
39Kwa hivyo, Malaika wakamwita hali ya kuwa amesimama katika chumba akisali kwamba: Mwenyezi Mungu anakupa bishara njema ya Yahya, atakayesadikisha neno litokalo kwa Mwenyezi Mungu, na ni bwana, na mtawa, na ni Nabii miongoni mwa walio wema.
40Zakariya akasema: Mola wangu Mlezi! Vipi nitapata mwana, ilhali tayari uzee umeshanifikia, na mke wangu ni tasa? Akasema: Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu, yeye hufanya apendavyo.
41Akasema: Mola wangu Mlezi! Niwekee alama. Akasema: Alama yako ni kuwa hutasema na watu kwa siku tatu, isipokuwa kwa kuashiria tu. Na mtaje Mola wako Mlezi kwa wingi, na mtakase jioni na asubuhi.
42Na tazama, pale Malaika waliposema: Ewe Maryam! Kwa hakika, Mwenyezi Mungu amekuteua, na amekutakasa, na amekuteua juu ya wanawake wa walimwengu wote.
43Ewe Maryam! Mnyenyekee Mola wako Mlezi, na usujudu, na urukuu pamoja na wanaorukuu.
44Hizi ni katika habari za ghaibu tunazokufunulia. Nawe hukuwa nao walipokuwa wakitupa kalamu zao ni nani wao atakayemlea Maryam? Na hukuwa nao walipokuwa wakizozana.
45Pale Malaika waliposema: Ewe Maryam! Hakika, Mwenyezi Mungu anakupa bishara njema ya (mwana kwa) neno litokalo kwake. Jina lake ni Masihi Isa mwana wa Maryam, mwenye heshima katika dunia na Akhera, na ni miongoni mwa waliowekwa karibu (na Mwenyezi Mungu).
46Naye atazungumza na watu katika utoto wake na katika utu uzima wake, na atakuwa katika walio wema.
47Maryam akasema: Mola wangu Mlezi! Vipi nitampata mwana ilhali hajanigusa mwanadamu? Akasema: Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu, yeye huumba atakavyo. Anapohukumu jambo, yeye kwa hakika huliambia: 'Kuwa!' Na linakuwa.
48Na atamfundisha kuandika na hekima na Taurati na Injili.
49Na ni Mtume kwa Wana wa Israili kuwaambia: Mimi kwa hakika nimewajia na Ishara kutoka kwa Mola wenu Mlezi, ya kwamba mimi kwa hakika ninawaundia kwa udongo kama sura ya ndege. Kisha ninapuliza ndani yake na anakuwa ndege kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Na ninawaponesha vipofu wa tangu kuzaliwa na wakoma, na ninawafufua maiti kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Na ninawaambia mnachokila na mnachoweka akiba katika nyumba zenu. Hakika, katika haya ipo Ishara kwenu ikiwa nyinyi ni Waumini.
50Na ninasadikisha yaliyokuwa kabla yangu katika Taurati, na ili niwahalalishie baadhi ya yale mliyoharamishiwa. Na nimewajia na Ishara kutoka kwa Mola Mlezi wenu. Kwa hivyo, mcheni Mwenyezi Mungu na nitiini mimi.
51Hakika, Mwenyezi Mungu ni Mola wangu Mlezi na ni Mola wenu Mlezi. Basi muabuduni Yeye. Hii ndiyo Njia iliyonyooka.
52Isa alipohisi ukafiri miongoni mwao, akasema: Ni nani watakaonisaidia katika kulingania kwa Mwenyezi Mungu? Wanafunzi wake wakasema: Sisi tutamnusuru Mwenyezi Mungu. Tumemuamini Mwenyezi Mungu, na shuhudia kwamba sisi hakika ni Waislamu.
53Mola wetu Mlezi! Tuliyaamini uliyoyateremsha, na tulimfuata Mtume huyu, basi tuandike pamoja na wanaoshuhudia.
54Na makafiri wakapanga vitimbi, na Mwenyezi Mungu akapanga vitimbi, na Mwenyezi Mungu ndiye mbora wa wenye kupanga vitimbi.
55Pale Mwenyezi Mungu aliposema: Ewe Isa, hakika Mimi nitakuchukua (bila kukufisha), na nitakunyanyua hadi kwangu, na nitakutakasa kutokana na wale waliokufuru, na nitawaweka wale waliokufuata juu ya wale waliokufuru, mpaka Siku ya Kiyama. Kisha kwangu ndiko marejeo yenu, na nihukumu kati yenu katika yale mliyokuwa mkihitilafiana.
56Ama wale waliokufuru, basi nitawaadhibu adhabu kali katika dunia na Akhera, na wala hawatapata wowote wa kuwanusuru.
57Na ama wale walioamini na wakatenda mema, basi Mwenyezi Mungu atawalipa ujira wao kamili. Na Mwenyezi Mungu hawapendi madhalimu.
58Haya tunayokusomea ni katika Aya na ukumbusho wenye hekima.
59Hakika, mfano wa Isa kwa Mwenyezi Mungu ni kama mfano wa Adam. Alimuumba kwa udongo kisha akamwambia: 'Kuwa!' Basi akawa.
60Hii ni haki itokayo kwa Mola wako Mlezi. Basi usiwe miongoni mwa wanaofanya shaka.
61Basi mwenye kukuhoji katika haya baada ya yale yaliyokufikia katika elimu hii, waambie: Njooni tuwaite watoto wetu na watoto wenu, na wake zetu na wake zenu, na sisi wenyewe na nyinyi wenyewe, kisha tuombe kwa unyenyekevu tutake laana ya Mwenyezi Mungu iwashukie waongo.
62Hakika, haya ndiyo maelezo ya kweli. Na hakuna mungu yeyote isipokuwa Mwenyezi Mungu tu. Na hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hekima.
63Na wakigeuka, basi Mwenyezi Mungu anawajua mno waharibifu.
64Sema: 'Enyi Watu wa Kitabu! Njooni kwenye neno lililo sawa baina yetu na nyinyi: Ya kwamba tusimuabudu yeyote isipokuwa Mwenyezi Mungu, wala tusimshirikishe na chochote. Wala tusifanyane waungu sisi kwa sisi badala ya Mwenyezi Mungu.' Na wakigeuka, basi semeni: Shuhudieni ya kwamba sisi kwa hakika ni Waislamu.
65Enyi Watu wa Kitabu! Mbona mnabishana juu ya Ibrahim, na hali Taurati na Injili havikuteremshwa isipokuwa baada yake? Kwani hamtumii akili?
66Angalieni! Nyinyi mlibishana katika yale mliyoyajua. Mbona sasa mnabishana katika yale msiyoyajua? Na Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye, na nyinyi hamjui.
67Ibrahim hakuwa Myahudi wala Mkristo. Lakini alikuwa mnyoofu, Muislamu, na wala hakuwa katika washirikina.
68Hakika, watu wanaomstahiki zaidi Ibrahim ni wale waliomfuata yeye, na Nabii huyu na wale walioamini. Na Mwenyezi Mungu ndiye Kipenzi Mlinzi wa Waumini.
69Kilipenda kikundi katika Watu wa Kitabu lau kuwa wangekupotezeni. Lakini hawapotezi isipokuwa nafsi zao, nao wenyewe hawatambui.
70Enyi Watu wa Kitabu! Kwa nini mnazikufuru Ishara za Mwenyezi Mungu ilhali nyinyi mnashuhudia?
71Enyi Watu wa Kitabu! Kwa nini mnaivisha haki uongo, na mnaificha haki ilhali mnajua?
72Na kilisema kikundi kimoja katika Watu wa Kitabu: Yaaminini yale waliyoteremshiwa wale walioamini mwanzo wa mchana, na yakufuruni mwisho wake; huenda wakarejea.
73Wala msimuamini isipokuwa yule anayeifuata dini yenu. Sema: Hakika uongofu ni uongofu wa Mwenyezi Mungu, kuwa apewe mtu mfano wa yale mliyopewa nyinyi au wawahoji mbele ya Mola wenu Mlezi. Sema: Hakika fadhila zimo mkononi mwa Mwenyezi Mungu. Humpa hizo amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye wasaa, Mwenye kujua.
74Yeye humchagua kumpa rehema zake amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye fadhila kubwa.
75Na miongoni mwa Watu wa Kitabu yupo ambaye ukimpa amana ya mrundo wa mali, atakurudishia. Na miongoni mwao yupo ambaye ukimpa amana ya dinari moja, hakurudishii isipokuwa ukimsimamia kumdai. Haya ni kwa kuwa walisema: 'Hatuna lawama kwa sababu ya hawa wasiojua kusoma na kuandika.' Na wanasema uongo juu ya Mwenyezi Mungu hali ya kuwa wanajua.
76Sivyo hivyo! Bali mwenye kulitimiza agano lake na akawa mcha Mungu, basi hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wacha Mungu.
77Hakika, wale wanaouza agano la Mwenyezi Mungu na viapo vyao kwa thamani ndogo, hao hawatakuwa na fungu lolote katika Akhera, wala Mwenyezi Mungu hatasema nao, wala hatawatazama Siku ya Kiyama, wala hatawatakasa, nao wana adhabu chungu.
78Na hakika wapo miongoni mwao kundi lipindualo ndimi zao katika kusoma Kitabu ili mdhani kuwa hayo yanatoka Kitabuni, na wala hayatoki Kitabuni. Nao husema: 'Haya yametoka kwa Mwenyezi Mungu.' Na wala hayakutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na wanasema uongo juu ya Mwenyezi Mungu hali ya kuwa wanajua.
79Haikumfailia mtu yeyote kwamba Mwenyezi Mungu ampe Kitabu na hekima na Unabii, kisha awaambie watu: 'Kuweni wa kuniabudu mimi badala ya Mwenyezi Mungu.' Bali atawaambia: 'Kuweni wenye kumuabudu Mola Mlezi wa viumbe vyote, kwa kuwa nyinyi mnafundisha Kitabu na kwa kuwa mnakisoma.'
80Wala hatawaamrisha kwamba muwafanye Malaika na Manabii kuwa ni miungu. Je, atawaamrisha ukafiri baada ya nyinyi kuwa Waislamu?
81Na pale Mwenyezi Mungu alipochukua agano la Manabii: Nikishawapa Kitabu na hekima, kisha akawajia Mtume mwenye kusadikisha yale mliyo nayo, basi hakika mtamuamini na mtamsaidia. Akasema: Je, mmekiri na mmekubali kushika agano langu la mkazo juu ya hayo? Wakasema: Tumekubali. Akasema: Basi shuhudieni, na Mimi ni pamoja nanyi katika wanaoshuhudia.
82Kwa hivyo, mwenye kugeuka baada ya haya, basi hao ndio wavukao mipaka.
83Je, wanataka dini isiyokuwa ya Mwenyezi Mungu, ilhali kila kilicho katika mbingu na katika ardhi kimejisalimisha kwake kwa kumtii Yeye kwa kupenda na kwa kutopenda, na kwake Yeye watarejeshwa?
84Sema: Tumemwamini Mwenyezi Mungu, na yale tuliyoteremshiwa sisi, na yale yaliyoteremshwa kwa Ibrahim, na Ismail, na Is-haak na Yaakub na wana wake, na yale aliyopewa Musa na Isa na Manabii wengine kutoka kwa Mola wao Mlezi. Hatutofautishi yeyote baina yao, na sisi ni wenye kujisalimisha kwake.
85Na mwenye kutafuta dini isiyokuwa Uislamu, basi haitakubaliwa kutoka kwake. Naye katika Akhera atakuwa miongoni mwa waliohasirika.
86Vipi Mwenyezi Mungu atawaongoa kaumu waliokufuru baada ya kuamini kwao, na wakashuhudia ya kuwa Mtume huyu ni wa haki, na zikawajia hoja zilizo wazi? Na Mwenyezi Mungu hawaongoi kaumu ya madhalimu.
87Hao malipo yao ni kuwa ipo juu yao laana ya Mwenyezi Mungu na ya Malaika na ya watu wote.
88Humo watadumu. Hawatapunguziwa adhabu, wala hawatapewa nafasi.
89Isipokuwa wale waliotubu baada ya hayo na wakatengenea. Basi Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.
90Hakika, wale waliokufuru baada ya kuamini kwao, kisha wakazidi kukufuru, haitakubaliwa toba yao, na hao ndio waliopotea.
91Hakika, wale waliokufuru, na wakafa hali ya kuwa ni makafiri, haitakubaliwa kutoka kwa yeyote wao fidia ya dhahabu ya kujaza dunia nzima lau wangeliitoa. Hao wana adhabu chungu, wala hawatakuwa na wowote wa kuwanusuru.
92Kamwe hamtaufikia wema mpaka mtoe katika vile mnavyovipenda. Na kitu chochote mnachokitoa, basi hakika Mwenyezi Mungu anakijua vyema.
93Kila chakula kilikuwa halali kwa Wana wa Israili isipokuwa kile alichojiharamishia Israili mwenyewe kabla ya kuteremshwa Taurati. Sema: Ileteni Taurati, na muisome ikiwa nyinyi ni wakweli.
94Na mwenye kumzulia uongo Mwenyezi Mungu baada ya hayo, basi hao ndio madhalimu.
95Sema: Mwenyezi Mungu amesema kweli. Basi fuateni mila ya Ibrahim mwongofu, wala hakuwa miongoni mwa washirikina.
96Hakika, Nyumba ya kwanza waliyowekewa watu kwa ibada ni ile iliyo Bakka, iliyobarikiwa na yenye uongofu kwa walimwengu.
97Ndani yake kuna Ishara zilizo wazi - masimamio ya Ibrahim. Na mwenye kuingia humo, anakuwa na amani. Na kwa ajili ya Mwenyezi Mungu imewawajibikia watu wahiji kwenye Nyumba hiyo, kwa yule awezaye njia ya kuiendea. Na atakayekufuru, basi hakika Mwenyezi Mungu si mhitaji kwa walimwengu.
98Sema: Enyi Watu wa Kitabu! Kwa nini mnazikufuru ishara za Mwenyezi Mungu, na ilhali Mwenyezi Mungu ni Shahidi kwa yote mnayoyatenda?
99Sema: Enyi Watu wa Kitabu! Kwa nini mnamzuilia Njia ya Mwenyezi Mungu aliyeamini mkiitakia ipotoke, ilhali nyinyi mnashuhudia? Na Mwenyezi Mungu si mwenye kughafilika mbali na mnayoyatenda.
100Enyi mlioamini! Mkilitii kundi katika wale waliopewa Kitabu, watawarudisha baada ya kuamini kwenu muwe makafiri.
101Na vipi mkufuru hali ya kuwa nyinyi mnasomewa Aya za Mwenyezi Mungu, na Mtume wake yuko miongoni mwenu? Na mwenye kushikamana na Mwenyezi Mungu, basi huyo hakika ameongolewa kwenye Njia iliyonyooka.
102Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu haki ya kumcha, wala kamwe msife isipokuwa nyinyi ni Waislamu.
103Na shikamaneni kwa Kamba ya Mwenyezi Mungu nyote pamoja, wala msitengane. Na ikumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu juu yenu: Mlipokuwa maadui nyinyi kwa nyinyi, naye akaziunganisha nyoyo zenu; na kwa neema yake mkawa ndugu. Na mlikuwa kwenye ukingo wa shimo la Moto, naye akawaokoa kutokana nao. Hivi ndivyo Mwenyezi Mungu anavyowabainishia Ishara zake ili mpate kuongoka.
104Na uwepo umma miongoni mwenu wanaoilingania heri, na wanaamrisha mema na wanakataza maovu. Na hao ndio waliofaulu.
105Wala msiwe kama wale waliotengana na wakahitilafiana baada ya kufikiwa na hoja zilizo wazi. Na hao ndio wana adhabu kubwa.
106Siku ambapo nyuso zitakuwa nyeupe, na nyuso nyingine zikawa nyeusi. Basi, ama wale ambao nyuso zao zitakuwa nyeusi (wataambiwa): Je, mlikufuru baada ya kuamini kwenu? Basi ionjeni adhabu kwa sababu ya yale mliyokuwa mkikufuru.
107Na ama wale ambao nyuso zao zitakuwa nyeupe, basi watakuwa katika rehema ya Mwenyezi Mungu. Wao humo watadumu.
108Hizi ni Aya za Mwenyezi Mungu tunazokusomea kwa haki. Na Mwenyezi Mungu hataki kuwadhulumu walimwengu.
109Na ni cha Mwenyezi Mungu kilicho katika mbingu na kilicho katika ardhi, na kwa Mwenyezi Mungu ndiko mambo yote yatarejeshwa.
110Nyinyi mmekuwa bora ya umma waliotolewa watu, kwa kuwa mnaamrisha mema na mnakataza maovu, na mnamuamini Mwenyezi Mungu. Na lau kuwa Watu wa Kitabu waliamini, ingelikuwa bora kwao. Miongoni mwao wako Waumini, lakini wengi wao ni wavukao mipaka.
111Maadui hawatawadhuru isipokuwa kwa maudhi tu. Na wakipigana nanyi, watawapa migongo, kisha hawatanusuriwa.
112Umepigwa udhalilifu juu yao popote wanapokutwa, isipokuwa kwa kamba ya Mwenyezi Mungu na kamba ya watu. Na walirudi na ghadhabu kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na unyonge umepigwa juu yao. Hayo ni kwa sababu walikuwa wakizikufuru Ishara za Mwenyezi Mungu, na wakiwaua Manabii bila ya haki. Hayo ni kwa sababu waliasi na walikuwa wakiruka mipaka.
113Wote hao si wamoja. Miongoni mwa Watu wa Kitabu kuna watu waliosimama barabara, wanasoma Aya za Mwenyezi Mungu nyakati za usiku, nao wanasujudu.
114Wanamwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho, na wanaamrisha mema na wanakataza maovu, na wanakimbilia katika mambo ya heri. Na hao wako miongoni mwa walio wema.
115Na heri yoyote wanayoifanya, basi hawatanyimwa malipo yake. Na Mwenyezi Mungu anawajua wacha Mungu.
116Hakika, wale waliokufuru, hazitawafaa kitu mali zao wala watoto wao mbele ya Mwenyezi Mungu. Na hao ndio watu wa Motoni. Wao watadumu humo.
117Mfano wa vile wanavyovitoa katika uhai wao wa duniani ni kama upepo ambao ndani yake kuna baridi ya barafu, ukalipiga shamba la kaumu waliozidhulumu nafsi zao, basi ukaliharibu. Na Mwenyezi Mungu hakuwadhulumu, bali wao wenyewe wanazidhulumu nafsi zao.
118Enyi mlioamini! Msiwafanye wandani wenu kuwa watu wasiokuwa katika nyinyi. Hawataacha kuwafikishia lolote la kuwadhuru. Wanapenda mngepata taabu. Imekwishadhihirika chuki yao kutoka katika midomo yao. Na yanayofichwa na vifua vyao ni makubwa zaidi.Tumekwishawabainishia Ishara ikiwa nyinyi mnatumia akili.
119Nyinyi ndio hawa mnawapenda watu hao, wala wao hawawapendi. Nanyi mnaviamini Vitabu vyote. Na wanapokutana nanyi husema: 'Tumeamini.' Na wanapokuwa peke yao, wanawaumia vidole kwa chuki. Sema: Kufeni na chuki yenu! Hakika, Mwenyezi Mungu anayajua vyema yale yaliyo katika vifua.
120Ikikuguzeni heri, inawawia vibaya. Na ikikupateni shari, wanaifurahia. Na nyinyi mkisubiri na mkamcha Mwenyezi Mungu, havitawadhuru kitu vitimbi vyao. Hakika, Mwenyezi Mungu ameyazingira yote wayatendayo.
121Na pale ulipotoka asubuhi kwa ahali zako ili uwapange Waumini kwenye vituo kwa ajili ya vita. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.
122Makundi mawili miongoni mwenu yalipoingiwa na woga kuwa watashindwa - na hali Mwenyezi Mungu ndiye Kipenzi Mlinzi wao. Na kwa Mwenyezi Mungu tu, na wategemee Waumini.
123Na Mwenyezi Mungu alishawanusuru huko Badri hali ya kuwa nyinyi ni wanyonge. Basi mcheni Mwenyezi Mungu ili mpate kushukuru.
124Ulipowaambia Waumini: Je, haiwatoshi kwamba Mola wenu Mlezi awasaidie kwa Malaika elfu tatu walioteremshwa?
125Kwani! Ikiwa mtavumilia na mkamcha Mungu, na hata maadui wakiwajia mara hii, basi hapo Mola wenu Mlezi atakusaidieni kwa Malaika elfu tano wenye alama maalumu.
126Na Mwenyezi Mungu hakufanya haya isipokuwa iwe ni bishara kwenu, na ili nyoyo zenu zipate kutua kwa hilo. Na nusura haitoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye Nguvu, Mwenye hekima.
127Ili akate sehemu katika wale waliokufuru, au awahizi; wapate kurejea nyuma hali ya kuwa wameambulia patupu.
128Wewe huna chochote katika jambo hili. Ama atawakubalia toba au atawaadhibu, kwani wao hakika ni madhalimu.
129Na ni vya Mwenyezi Mungu vyote vilivyo katika mbingu na vilivyo katika ardhi. Yeye humfutia dhambi amtakaye na humwadhibu amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kufuta dhambi, Mwenye kurehemu.
130Enyi mlioamini! Msile riba mkizidisha juu kwa juu. Na mcheni Mwenyezi Mungu ili mpate kufaulu.
131Na ucheni Moto ambao umeandaliwa kwa ajili ya makafiri.
132Na mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume ili mpate kurehemewa.
133Na kimbilieni kufutiwa dhambi kutoka kwa Mola wenu Mlezi, na Bustani ambayo upana wake ni mbingu na ardhi. Iliandaliwa kwa ajili ya wacha Mungu.
134Wale ambao hutoa wanapokuwa katika nyakati nzuri na wanapokuwa katika dhiki, na wanajizuia ghadhabu, na ni wasamehevu kwa watu. Na Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao wema.
135Na wale ambao wanapofanya uchafu au wakazidhulumu nafsi zao, humtaja Mwenyezi Mungu; na hapo wanamwomba kufutiwa dhambi zao. Na ni nani anayefuta dhambi isipokuwa Mwenyezi Mungu? Na wala hawaendelei na waliyoyafanya hali ya kuwa wanajua.
136Hao malipo yao ni kufutiwa dhambi kutoka kwa Mola wao Mlezi, na Bustani zipitazo mito chini yake. Humo watadumu, na bora zaidi ni ujira wa watendao (wema).
137Tayari zimepita kabla yenu nyendo nyingi. Basi tembeeni katika ulimwengu na muangalie vipi ulikuwa mwisho wa wanaokanusha.
138Huu ni ubainisho kwa watu wote, na ni uongofu, na mawaidha kwa wacha Mungu.
139Wala msilegee, wala msihuzunike, kwani nyinyi ndio wa juu ikiwa nyinyi ni Waumini.
140Ikiwa mtaguswa na majeraha, basi kwa hakika hao watu wengine walikwishapatwa na majeraha mfano wake. Na siku za namna hii tunawaletea watu kwa zamu, ili Mwenyezi Mungu awajue wale walioamini na awateue miongoni mwenu wanaokufa kwa ajili ya Dini (Mashahidi). Na Mwenyezi Mungu hawapendi madhalimu.
141Na pia ili Mwenyezi Mungu awasafishe walioamini na awafutilie mbali makafiri.
142Je, mnadhani kwamba mtaingia Bustanini ilhali Mwenyezi Mungu hajawajua wale miongoni mwenu waliopigana Jihadi, na akawajua waliosubiri?
143Na nyinyi mlikuwa mkiyatamani mauti kabla hamjakutana nayo. Basi sasa mmekwishayaona na huku mnayatazama.
144Na Muhammad si isipokuwa Mtume tu. Wamekwishapita kabla yake Mitume. Je, akifa au akiuawa, mtageuka mrudi kwa visigino vyenu? Na atakayegeuka akarudi kwa visigino vyake, basi huyo hatamdhuru kitu Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu atawalipa wanaoshukuru.
145Na haikuwa kwa nafsi kufa isipokuwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu kama ilivyoandikiwa muda wake. Na mwenye kutaka malipo ya duniani, tutampa kwayo. Na mwenye kutaka malipo ya Akhera, tutampa kwayo. Na tutawalipa wenye kushukuru.
146Na ni Manabii wangapi ambao Waumini wengi wenye ikhlasi walipigana vita pamoja nao! Na hawakulegea kwa yaliyowapata katika Njia ya Mwenyezi Mungu, wala hawakudhoofika wala hawakusalimu amri. Na Mwenyezi Mungu huwapenda wanaosubiri.
147Na haikuwa kauli yao isipokuwa walisema: Mola wetu Mlezi! Tufutie dhambi zetu na kupita kwetu kiasi katika mambo yetu, na isimamishe imara miguu yetu na utunusuru dhidi ya kaumu ya makafiri.
148Basi Mwenyezi Mungu akawapa malipo ya duniani na malipo bora ya Akhera. Na Mwenyezi Mungu anawapenda wafanyao mema.
149Enyi mlioamini! Ikiwa mtawatii wale waliokufuru, watawarudisha kwa visigino vyenu, na hapo mtageuka huku mmehasirika.
150Bali Mwenyezi Mungu ndiye Kipenzi Mlinzi wenu. Naye ndiye mbora wa wanaonusuru.
151Tutatia hofu katika nyoyo za wale waliokufuru kwa vile walivyomshirikisha Mwenyezi Mungu na yale ambayo hakuyateremshia hoja yoyote. Na makazi yao ni Motoni. Na maovu mno ni maskani ya madhalimu!
152Na Mwenyezi Mungu aliwatimilizia ahadi yake, vile mlivyokuwa mnawaua kwa idhini yake, mpaka mlipolegea na mkazozana katika amri hii, na mkaasi baada ya Yeye kuwaonyesha yale mnayoyapenda. Wapo miongoni mwenu wanaotaka dunia, na wapo miongoni mwenu wanaotaka Akhera. Kisha akawatenga nao (maadui) ili akujaribuni. Naye sasa amekwishawasamehe. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye fadhila juu ya Waumini.
153Pale mlipokuwa mkikimbia mbio, wala hamumsikilizi yeyote, na Mtume anawaita, yuko nyuma yenu. Basi Mwenyezi Mungu akawapa dhiki juu ya dhiki, ili msisikitike kwa yale yaliyowakosa wala kwa yale yaliyowapata. Na Mwenyezi Mungu ana habari za yote mnayoyatenda.
154Kisha baada ya dhiki aliwateremshia utulivu - usingizi ambao ulifunika kundi moja kati yenu. Na kundi jingine nafsi zao ziliwashughulisha hata wakamdhania Mwenyezi Mungu dhana isiyokuwa ya haki, dhana ya kijinga. Wakisema: Je, sisi tuna lolote katika jambo hili? Sema: Jambo hili lote ni la Mwenyezi Mungu. Wanaficha katika nafsi zao wasiyokudhihirishia. Wanasema: Lau ingelikuwa tuna lolote katika jambo hili, tusingeuliwa papa hapa. Sema: Hata mngelikuwa majumbani mwenu, basi wangelitoka wale walioandikiwa kufa, wakaenda mahali pao pa kuangukia wafe. (Haya ni hivyo) ili Mwenyezi Mungu ayajaribu yaliyo katika vifua vyenu, na asafishe yaliyo katika nyoyo zenu. Na Mwenyezi Mungu anayajua vyema yaliyomo vifuani.
155Hakika, wale waliogeuka wakakimbia miongoni mwenu siku yalipokutana makundi mawili, hakika Shetani tu ndiye aliyewatelezesha kwa sababu ya baadhi ya makosa waliyoyafanya. Na Mwenyezi Mungu amekwishawasamehe. Hakika, Mwenyezi Mungu ni Mwenye kufuta dhambi, Mpole.
156Enyi mlioamini! Msiwe kama wale waliokufuru na wakawaambia ndugu zao wanaposafiri katika nchi au wanapokuwa vitani: 'Lau wangelikuwa nasi, wasingelikufa na wasingeliuwawa.' Ili Mwenyezi Mungu afanye hayo kuwa ni majuto makubwa katika nyoyo zao. Na Mwenyezi Mungu huhuisha na hufisha. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyaona vyema mnayoyatenda.
157Na mkiuliwa katika Njia ya Mwenyezi Mungu, au mkifa, hakika kufutiwa dhambi kutoka kwa Mwenyezi Mungu na rehema ni bora kuliko yale wanayoyakusanya.
158Na mkifa au mkiuliwa, basi ni kwa Mwenyezi Mungu ndiko mtakakokusanywa.
159Basi ni kwa sababu ya rehema itokayo kwa Mwenyezi Mungu ndiyo umekuwa laini kwao. Na lau ungelikuwa mkali, mwenye moyo mgumu, bila ya shaka wangelikukimbia. Basi wasamehe, na waombee kufutiwa dhambi, na shauriana nao katika mambo. Na ukishakata shauri, basi mtegemee Mwenyezi Mungu. Hakika, Mwenyezi Mungu huwapenda wanaomtegemea.
160Ikiwa Mwenyezi Mungu atakunusuruni, basi hakuna wa kukushindeni. Na akikutupeni, basi ni nani huyo baada yake atakayekunusuruni? Na kwa Mwenyezi Mungu tu, basi na wategemee Waumini.
161Na haikuwa kwa Nabii yeyote kufanya hiyana. Na atakayefanya hiyana, atakuja Siku ya Kiyama na kile alichofanyia hiyana, kisha kila nafsi italipwa kwa iliyoyachuma kwa ukamilifu; wala hawatadhulumiwa.
162Je, aliyeyafuata ya kumridhisha Mwenyezi Mungi ni kama yule aliyerudi na ghadhabu ya Mwenyezi Mungu, na makazi yake yakawa Jahannamu? Napo ndipo pahali pabaya mno pa kurejea.
163Hao wana vyeo mbalimbali kwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyaona yote wayatendayo.
164Hakika, Mwenyezi Mungu amewafanyia wema mkubwa Waumini alipowaletea Mtume kutoka miongoni mwao wenyewe, anayewasomea Aya zake, na anawatakasa, na anawafunza Kitabu na hekima, ijapokuwa kabla ya hapo walikuwa katika upotovu ulio wazi.
165Nyinyi mlipopatwa na msiba ambao nyinyi mmekwishawatia mara mbili mfano wake, mkasema: Umetoka wapi huu? Sema: Huo umetoka kwenu wenyewe. Hakika, Mwenyezi Mungu ni Mwenye uwezo juu ya kila kitu.
166Na yale yaliyowapata siku yalipokutana makundi mawili, yalikuwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, na ili awajue Waumini.
167Na ili awajue wale waliofanya unafiki, walipoambiwa: Njooni mpigane katika Njia ya Mwenyezi Mungu au lindeni. Wakasema: 'Tungelijua kuna kupigana vita, bila ya shaka tungeliwafuata.' Wao siku ile walikuwa karibu zaidi na ukafiri kuliko Imani. Wanasema kwa midomo yao yasiyokuwa katika nyoyo zao. Na Mwenyezi Mungu anajua vyema wanayoyaficha.
168Wale waliowaambia ndugu zao, na wao wenyewe walikuwa wamekaa: Lau wangelitutii, wasingeliuliwa. Sema: Ziondoleeni nafsi zenu mauti kama nyinyi ni wakweli.
169Wala kabisa usiwadhanie wale waliouliwa katika Njia ya Mwenyezi Mungu kuwa ni wafu. Bali hao wa hai kwa Mola wao Mlezi wanaruzukiwa.
170Wanafurahia yale aliyowapa Mwenyezi Mungu katika fadhila zake, na wanawapa bishara wale ambao bado hawajajiunga nao, walio nyuma yao, ya kwamba haitakuwa hofu juu yao wala hawatahuzunika.
171Wanapata bishara ya neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu na fadhila, na ya kwamba Mwenyezi Mungu hapotezi ujira wa Waumini.
172Wale waliomwitikia Mwenyezi Mungu na Mtume baada ya kwishapatwa na majeraha. Kwa waliofanya wema miongoni mwao na wakamcha Mungu, utakuwa ujira mkubwa.
173Wale walioambiwa na watu: 'Hakika, kuna watu wamewakusanyikia, hivyo waogopeni!' Hayo yakawazidishia Imani, na wakasema: Mwenyezi Mungu anatutosha, naye ni mbora zaidi wa kutegemewa.
174Basi wakarudi na neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu na fadhila. Hakuna baya lililowagusa, na wakafuata yanayomridhisha Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye fadhila kubwa.
175Hakika, huyo ni Shetani tu anawatia hofu marafiki zake. Basi msiwaogope. Bali niogopeni Mimi ikiwa nyinyi ni Waumini.
176Wala wasikuhuzunishe wale wanaoukimbilia ukafiri. Hakika, hao hawamdhuru kitu Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu anataka asiwawekee fungu lolote katika Akhera. Na wana adhabu kubwa.
177Hakika, wale walioununua ukafiri kwa Imani, hawatamdhuru kitu Mwenyezi Mungu. Na wana adhabu chungu.
178Wala wasidhani kabisa wale wanaokufuru kwamba muhula huu tunaowapa ni heri kwao. Hakika, tunawapa muhula ili wazidishe dhambi. Na wana adhabu ya kudunisha.
179Na hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwaacha Waumini katika hali mliyo nayo mpaka apambanue mbaya kutokana na mwema. Na wala hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwajulisha mambo ya ghaibu. Lakini Mwenyezi Mungu humteua katika Mitume wake amtakaye. Basi muaminini Mwenyezi Mungu na Mitume wake. Na mkiamini, na mkamcha Mungu, basi mtakuwa na ujira mkubwa.
180Wala wasidhani kabisa wale ambao wanafanya ubahili katika aliyowapa Mwenyezi Mungu katika fadhila zake kuwa ni heri kwao. Bali hiyo ni shari kwao. Watafungwa shingoni yale waliyoyafanyia ubahili Siku ya Kiyama. Na urithi wa mbingu na ardhi ni wa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ana habari za yote myatendayo.
181Hakika Mwenyezi Mungu amekwishasikia kauli ya wale waliosema: 'Hakika, Mwenyezi Mungu ni fakiri, na sisi ni matajiri.' Tutayaandika yale waliyoyasema, na pia kuwaua kwao Manabii bila ya haki, na tutawaambia Siku ya Kiyama: Onjeni adhabu ya kuunguza.
182Hayo ni kwa sababu ya iliyotanguliza mikono yenu, na kwamba Mwenyezi Mungu si mwenye kuwadhulumu waja.
183Waliosema: Hakika, Mwenyezi Mungu alituusia kwamba tusimwamini Mtume yeyote mpaka atujie na kafara inayoliwa na moto. Waambie: Walikujieni Mitume kabla yangu kwa hoja zilizo wazi na kwa hayo mnayosema. Basi kwa nini mliwaua ikiwa nyinyi ni wakweli?
184Na wakikukadhibisha, basi walikadhibishwa Mitume wengine kabla yako, waliokuja na hoja zilizo wazi, na Vitabu vyenye hekima, na Kitabu chenye nuru.
185Kila nafsi itaonja mauti. Na bila ya shaka mtapewa ujira wenu kamili Siku ya Kiyama. Na atakayeepushwa na Moto, na akaingizwa Bustanini, basi huyo hakika amefuzu. Na maisha ya dunia si kitu isipokuwa starehe ya udanganyifu.
186Bila shaka mtajaribiwa katika mali zenu, na nafsi zenu. Na bila ya shaka yoyote mtasikia udhia mwingi kutoka kwa wale waliopewa Kitabu kabla yenu na wale walioshirikisha. Na ikiwa mtasubiri na mkamcha Mungu, basi hakika hayo ni katika mambo ya kuazimia.
187Na pale Mwenyezi Mungu alipochukua agano la wale waliopewa Kitabu kuwa: 'Bila shaka mtawabainishia watu, na wala hamtakificha.' Lakini wakakitupa nyuma ya migongo yao, na wakanunua kwacho thamani ndogo. Basi ni kiovu mno hicho wanachokinunua.
188Kamwe usiwadhanie wale wanaofurahia yale waliyoyafanya, na wakapenda kwamba wasifiwe kwa yale ambayo hawakuyatenda. Basi kamwe usiwadhanie kuwa watasalimika kutokana na adhabu. Na wana adhabu chungu.
189Na ni wa Mwenyezi Mungu ufalme wa mbingu na ardhi. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye uwezo juu ya kila kitu.
190Hakika, katika kuumbwa mbingu na ardhi na kuhitilafiana usiku na mchana ziko Ishara kwa wenye akili ya hali ya juu.
191Ambao humkumbuka Mwenyezi Mungu hali ya kuwa wamesimama, na wameketi, na kwenye mbavu zao. Na hutafakari katika kuumbwa kwa mbingu na ardhi, wakisema: Mola wetu Mlezi! Hukuviumba hivi bure. Subhanaka (umetakasika)! Basi tukinge kutokana na adhabu ya Moto.
192Mola wetu Mlezi! Hakika, yule unayemwingiza Motoni, basi umemhizi. Na waliodhulumu hawana wasaidizi wowote.
193Mola wetu Mlezi! Hakika, sisi tumemsikia mwitaji akiita kwenye Imani kwamba: 'Muaminini Mola wenu Mlezi'; kwa hivyo, tukaamini. Basi tufutie dhambi zetu, na utufunikie makosa yetu, na utufishe pamoja na walio wema.
194Mola wetu Mlezi! Na tupe yale uliyotuahidi kwa Mitume wako, wala usituhizi Siku ya Kiyama. Hakika, Wewe huvunji miadi.
195Basi, Mola wao Mlezi akayakubali maombi yao akayajibu: Hakika Mimi, sipotezi matendo ya mfanya matendo yeyote miongoni mwenu, akiwa mwanamume au mwanamke, kwani ni nyinyi kwa nyinyi. Basi waliohama, na waliotolewa katika makazi yao, na wakaudhiwa katika Njia yangu, na wakapigana vita, na wakauliwa, kwa yakini Mimi nitawafunikia makosa yao; na kwa yakini nitawaingiza katika Mabustani yanayopita mito chini yake. Hizo ndizo thawabu zinazotoka kwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu kwake kuna thawabu njema kabisa.
196Kamwe kusiwadanganye kutangatanga kwa wale waliokufuru katika nchi.
197Hiyo ni starehe ndogo. Kisha makazi yao yatakuwa Jahannamu. Na ni pahali pabaya mno pa kupumzikia.
198Lakini wale waliomcha Mola wao Mlezi wana Mabustani yanayopita mito chini yake. Watadumu humo. Hayo ni makaribisho yao yatokayo kwa Mwenyezi Mungu. Na vilivyo kwa Mwenyezi Mungu ni bora kwa walio wema.
199Na hakika, miongoni mwa Watu wa Kitabu kuna wale wanaomwamini Mwenyezi Mungu na yaliyoteremshwa kwenu na yaliyoteremshwa kwao, wakimnyenyekea Mwenyezi Mungu. Hawanunui kwa Aya za Mwenyezi Mungu thamani ndogo. Hao wana ujira wao kwa Mola wao Mlezi. Hakika, Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhesabu.[1]
200Enyi mlioamini! Subirini, na vumilieni, na kuweni macho, na mcheni Mwenyezi Mungu, ili mpate kufaulu.