إبراهيم
Abraham • 52 ayahs • Meccan
بِسْمِ ٱللَّهِ ٱلرَّحْمَٰنِ ٱلرَّحِيمِ
1Alif Laam Raa.[1] Hiki ni Kitabu tulichokuteremshia ili uwatoe watu kwenye giza mbalimbali uwapeleke kwenye mwangaza, kwa idhini ya Mola wao Mlezi, uwafikishe kwenye Njia ya Mwenye nguvu, Msifika.
2Naye ni Mwenyezi Mungu ambaye ni vyake Yeye vyote vilivyo katika mbingu zote na katika ardhi. Na ole wao makafiri kwa adhabu kali!
3Wale wanaoupendelea uhai wa dunia kuliko Akhera, na wanawazuilia watu Njia ya Mwenyezi Mungu, na wanataka kuipotosha. Hao wako katika upotovu wa mbali.
4Na hatukumtuma Mtume yeyote isipokuwa kwa ulimi wa kaumu yake ili apate kuwabainishia. Basi Mwenyezi Mungu anampoteza amtakaye, na anamwongoa amtakaye. Naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.
5Na hakika tulimtuma Musa na miujiza yetu, tukamwambia: Watoe kaumu yako kwenye giza mbalimbali uwapeleke kwenye nuru. Na uwakumbushe siku za Mwenyezi Mungu. Hakika katika hayo zipo ishara kwa kila mwenye kusubiri sawasawa, mwenye kushukuru sana.
6Na Musa alipowaambia kaumu yake, "Kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu juu yenu pale alipowaokoa kutokana na watu wa Firauni waliokuwa wakiwatia adhabu mbaya kabisa, wakiwachinja wana wenu wanaume, na wakiwaacha hai wanawake wenu. Na katika hayo ulikuwa mtihani mkubwa unaotoka kwa Mola wenu Mlezi."
7Na alipotangaza Mola wenu Mlezi: Mkishukuru, hakika nitawazidishia. Na mkikufuru, basi adhabu yangu ni kali.
8Na Musa alisema: Mkikufuru nyinyi na wote walio katika dunia, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujitosha, Msifika.
9Je, hazikuwafikia habari za wale waliokuwa kabla yenu? Kaumu ya Nuhu, na 'Aadi, na Thamud, na wale waliokuwa baada yao, ambao hakuna awajuaye isipokuwa Mwenyezi Mungu? Mitume wao waliwajia na hoja zilizo wazi, na wao wakarudisha mikono yao kwenye vinywa vyao, wakasema: Hakika sisi tumeyakufuru hayo mliyotumwa nayo, na hakika sisi tuko katika shaka kubwa na hayo mnayotuitia.
10Mitume wao wakasema: Ati kuna shaka kuhusiana na Mwenyezi Mungu, Muumba mbingu na ardhi? Yeye anawaita ili awafutie madhambi yenu, na awape muhula mpaka muda uliowekwa. Wakasema: Nyinyi si chochote isipokuwa ni wanadamu tu kama sisi. Mnataka kutuzuilia mbali na yale waliyokuwa wakiabudu baba zetu. Basi tujieni na hoja iliyo wazi.
11Mitume wao wakawaambia: Sisi kweli si chochote isipokuwa ni wanadamu kama nyinyi. Lakini Mwenyezi Mungu humneemesha amtakaye katika waja wake. Wala sisi hatuwezi kuwaletea uthibitisho isipokuwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Na juu ya Mwenyezi Mungu basi na wategemee Waumini.
12Na tuna nini hata tusimtegemee Mwenyezi Mungu, na hali Yeye ametuongoa kwenye njia zetu. Na hakuna hakika tutayavumilia hayo maudhi mnayotuudhi nayo. Na juu ya Mwenyezi Mungu na wategemee wanaotegemea.
13Na wale waliokufuru wakawaambia Mitume wao: Hakika, tutawatoa katika nchi yetu, au lazima mtarudi katika mila yetu. Basi Mola wao Mlezi akawafunulia ufunuo (wahyi): Hakika tutawaangamiza madhalimu!
14Na hakika tutawaweka kukaa katika ardhi baada yao. Haya ni kwa anayehofu kusimamishwa mbele yangu, na akahofu ahadi yangu ya adhabu.
15Na wakaomba ushindi, na akashindwa kila jabari mkaidi.
16Nyuma yake iko Jahannamu, na atanyweshwa katika maji ya usaha.
17Awe anayagugumiza, wala hataweza kuyameza. Na mauti yatamjia kutokea kila upande, wala hatakufa. Na zaidi ya hayo itakuwepo adhabu nyengine kali.
18Mfano wa wale waliomkufuru Mola wao Mlezi, vitendo vyao ni kama jivu linalopeperushwa kwa nguvu za upepo katika siku ya upepo mkali. Hawawezi kupata chochote katika yale waliyoyachuma. Huko ndiko kupotea kwa mbali!
19Je, huoni kuwa Mwenyezi Mungu ameziumba mbingu na ardhi kwa Haki? Akitaka, anawaondoa na alete viumbe wapya!
20Na hilo kwa Mwenyezi Mungu si jambo gumu.
21Na wote watajitokeza mbele ya Mwenyezi Mungu. Wanyonge watawaambia wale waliotakabari: Hakika sisi tulikuwa wafwasi wenu; basi hebu mtuondolee kidogo hivi katika adhabu ya Mwenyezi Mungu? Watasema: Lau Mwenyezi Mungu angelituongoa, basi hakuna shaka nasi tungeliwaongoa. Ni mamoja kwetu tukipapatika au tukisubiri; hatuna popote pa kukimbilia.
22Na shetani atasema itakapokatwa hukumu: Hakika Mwenyezi Mungu aliwaahidi ahadi ya kweli. Nami niliwaahidi; lakini sikuwatimizia ahadi yangu. Na sikuwa na mamlaka yoyote juu yenu, isipokuwa niliwaita, nanyi mkaniitikia. Basi msinilaumu mimi, bali jilaumuni wenyewe. Mimi siwezi kuwa mtetezi wenu, wala nyinyi hamuwezi kuwa watetezi wangu. Hakika mimi nilikufuru tangu zamani huko kunishirikisha kwenu na Mwenyezi Mungu. Hakika madhalimu wana adhabu chungu.
23Na wale walioamini na wakatenda mema wataingizwa katika Mabustani yapitayo mito kwa chini yake, wadumu humo kwa idhini ya Mola wao Mlezi. Maamkizi yao humo yatakuwa: Salaam (Amani)!
24Je, hukuona vipi Mwenyezi Mungu alivyopiga mfano wa neno zuri? Ni kama mti mzuri, mizizi yake ni imara, na matawi yake yako mbinguni.
25Hutoa matunda yake kila wakati kwa idhini ya Mola wake Mlezi. Na Mwenyezi Mungu huwapigia watu mifano ili wapate kukumbuka.
26Na mfano wa neno ovu ni kama mti muovu, uliong'olewa juu ya ardhi. Hauna uimara wowote.
27Mwenyezi Mungu huwaimarisha wale walioamini kwa kauli ya imara katika uhai wa dunia na katika Akhera. Na Mwenyezi Mungu huwapoteza madhalimu. Na Mwenyezi Mungu hufanya apendavyo.
28Je, hukuwaona wale waliobadilisha neema ya Mwenyezi Mungu kwa kufuru, na wakawafikisha kaumu yao kwenye nyumba ya maangamizo?
29Nayo ni Jahannamu wataiingia! Na ni mahali pa kukaa pabaya mno!
30Na walimfanyia Mwenyezi Mungu wenza ili wapoteze watu kutoka kwenye njia yake. Sema: Stareheni! Kwani maishio yenu ni Motoni!
31Waambie waja wangu walioamini, wadumishe Swala, na watoe katika tulivyowaruzuku, kwa siri na dhahiri, kabla ya kufika kwa Siku isiyokuwa na biashara yoyote wala urafiki wa dhati.
32Mwenyezi Mungu ndiye aliyeziumba mbingu na ardhi, na akateremsha maji kutoka mbinguni, na kwa hayo akatoa matunda kuwa ni riziki yenu. Na akawatiishia majahazi yanayokwenda baharini kwa amri yake, na akawatiishia mito.
33Na akawatiishia jua na mwezi vinavyokwenda daima dawamu, na akawatiishia usiku na mchana.
34Na akawapa katika kila mlichomuomba. Na mkihesabu neema za Mwenyezi Mungu, hamuwezi kuzidhibiti. Hakika mwanadamu ni dhalimu mkubwa, mwenye kukufuru sana neema.
35Na Ibrahim aliposema: Ewe Mola wangu Mlezi! Ujaalie mji huu uwe wa amani, na uniepushe mimi na wanangu na kuabudu masanamu.
36Ewe Mola wangu Mlezi! Hakika hayo yamewapoteza wengi wa watu. Basi aliyenifuata mimi, huyo hakika ni miongoni mwangu. Na aliyeniasi, hakika Wewe ni Mwingi wa kusamehe, Mwingi wa kurehemu.
37Mola wetu Mlezi! Hakika mimi nimewaweka baadhi ya dhuria yangu katika bonde lisilokuwa na mimea, kwenye Nyumba yako Takatifu, ewe Mola wetu Mlezi, ili wadumishe Swala. Basi zifanye nyoyo za watu zielekee kwao, na waruzuku matunda, ili wapate kushukuru.
38Ewe Mola wetu Mlezi! Hakika Wewe unajua tunayoyaweka hadharani na tunayoyaficha. Na hakuna kitu kinachofichikana kwa Mwenyezi Mungu katika ardhi wala katika mbingu.
39Alhamdulillahi (sifa njema ni za Mwenyezi Mungu) aliyenitunuku pamoja na uzee wangu Ismail na Is-haq. Hakika Mola wangu Mlezi ni Mwenye kusikia sana maombi.
40Mola wangu Mlezi! Nifanye niwe mwenye kudumisha Swala, na katika dhuria yangu pia. Ewe Mola wetu Mlezi, na ikubali dua yangu.
41Mola wetu Mlezi! Nisamehe mimi na wazazi wangu wote wawili, na Waumini, siku itakaposimama hesabu.
42Wala kamwe usidhani Mwenyezi Mungu ameghafilika mbali na wanayoyafanya madhalimu. Hakika Yeye anawaahirisha tu mpaka siku yatakapokodoka macho yao.
43Watakuwa mbioni, vichwa juu, huku macho yao hayapepesi, na nyoyo zao zitakuwa tupu.
44Na waonye watu siku itakapowajia adhabu, na wale waliodhulumu waseme, "Ewe Mola wetu Mlezi! Tuahirishe muda kidogo tuitikie wito wako na tuwafuate Mitume." Kwani nyinyi hamkuapa zamani kwamba kamwe hamuwezi kuondoka?
45Na mkakaa katika maskani zile zile za wale waliozidhulumu nafsi zao. Na ikawabainikia jinsi tulivyowatendea. Nasi tukawapigia mifano mingi.
46Na hakika walifanya vitimbi vyao, na vitimbi vyao hivyo anavijua Mwenyezi Mungu. Na kwa yakini vitimbi vyao hivyo vilikuwa ni vya kuweza kuondosha milima.
47Basi kamwe usimdhanie Mwenyezi Mungu kuwa ni mwenye kuwavunjia ahadi yake Mitume wake. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye Nguvu, Mwenye kulipiza.
48Siku itakapogeuzwa ardhi iwe ardhi nyingine, na mbingu zote pia. Nao watajitokeza mbele ya Mwenyezi Mungu Mmoja, Mshindi.
49Na utaona wahalifu siku hiyo wamefungwa pamoja katika minyororo.
50Nguo zao zitakuwa za lami, na Moto utazigubika nyuso zao.
51Ili Mwenyezi Mungu ailipe kila nafsi yale iliyoyachuma. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhesabu.
52Huu ni ufikishaji kwa watu, ili waonywe kwao, na wapate kujua kuwa hakika Yeye ni Mungu Mmoja, na wapate kukumbuka wenye akili zilizo sawa.