الإسراء
The Night Journey • 111 ayahs • Meccan
بِسْمِ ٱللَّهِ ٱلرَّحْمَٰنِ ٱلرَّحِيمِ
1Ametakasika yule aliyemsafirisha mja wake usiku mmoja kutoka katika Msikiti Mtakatifu mpaka Msikiti wa Al-Aqswa, ambao tumebariki kandoni mwake, ili tumuonyeshe katika Ishara zetu. Hakika Yeye ndiye Mwenye kusikia zaidi, Mwenye kuona mno.
2Na tulimpa Musa Kitabu na tukakifanya kuwa ni uongofu kwa Wana wa Israili. (Tukawaambia) kwamba msimfanye yeyote asiyekuwa mimi kuwa mtegemewa wenu.
3Kizazi cha wale tuliowabeba pamoja na Nuhu. Hakika yeye alikuwa mja wa kushukuru sana.
4Na tukawahukumia Wana wa Israili katika Kitabu kwamba hakika mtafanya uharibifu katika ardhi mara mbili, na hakika mtapanda kiburi, kupanda kukubwa.
5Na itakapokuja ahadi ya kwanza yake, tutawatumia waja wetu wenye nguvu kubwa. Watawaingilia ndani ya majumba. Na hii ilikuwa ahadi iliyotimizwa.
6Kisha tukawarudishia nguvu zenu dhidi yao, na tukawasaidia kwa mali na wana, na tukawafanya kuwa wengi zaidi.
7Mkifanya wema, mnafanyia wema nafsi zenu. Na mkifanya ubaya, basi mnajifanyia wenyewe. Na ikifika ahadi ya mwisho ili waziharibu nyuso zenu na waingie Msikitini kama walivyoingia mara ya kwanza na waharibu kila walichokiteka kwa uharibifu mkubwa.
8Huenda Mola wenu Mlezi akakurehemuni, na mkirudia, na sisi tutarudia. Na tumeifanya Jahannam kuwa ni gereza kwa ajili ya makafiri.
9Hakika hii Qur-ani inaongoa kwenye yale yaliyonyooka kabisa, na inawabashiria Waumini ambao wanatenda mema ya kwamba wana malipo makubwa.
10Na ya kwamba wale wasioiamini Akhera, tumewaandalia adhabu chungu.
11Na mtu huomba maovu kama vile aombavyo heri, kwani mtu ni mwenye pupa mno.
12Na tumefanya usiku na mchana kuwa ishara mbili. Tena tukaifuta ishara ya usiku, na tukaifanya ishara ya mchana ni yenye mwangaza ili mtafute fadhila itokayo kwa Mola wenu Mlezi, na ili mpate kujua idadi ya miaka na hesabu. Na kila kitu tumekifafanua kwa kina waziwazi.
13Na kila mtu tumemfungia matendo yake shingoni mwake. Na Siku ya Kiyama tutamtolea kitabu atakachokikuta ki wazi kimekunjuliwa.
14Ataambiwa: Soma kitabu chako! Nafsi yako inakutosha leo kukuhesabu.
15Anayeongoka, basi anaongoka kwa ajili ya nafsi yake. Na anayepotea, basi anapotea kwa hasara yake mwenyewe. Wala habebi mbebaji mzigo wa mwengine. Wala Sisi hatuadhibu mpaka tumtume mtume.
16Na pindi tukitaka kuuteketeza mji, tunawaamrisha wale wana starehe na taanusi wake, lakini wao wakaendelea kutenda maovu humo. Basi hapo kauli ikathibiti juu ya mji huo, nasi tukauangamiza kwa maangamizo makubwa.
17Na kaumu ngapi tumeziangamiza baada ya Nuhu! Na Mola wako Mlezi anatosha kabisa kuwa ni Mwenye kuzijua na kuziona dhambi za waja wake.
18Anayetaka yapitayo upesi upesi, tutafanya haraka kumletea humo (duniani) tunayoyataka kwa tumtakaye. Kisha tumemwekea Jahannamu, ataingia humo hali ya kuwa ni mwenye kulaumiwa na kufurushwa.
19Na anayeitaka Akhera, na akaifanyia juhudi ipasavyo ilhali ni Muumini, basi hao juhudi zao zitakuwa ni za kushukuriwa.
20Wote hao tunawakunjulia, hawa na hao, katika vipawa vya Mola wako Mlezi. Wala vipawa vya Mola wako Mlezi havizuiliki.
21Angalia vipi tulivyowafadhilisha baadhi yao kuliko wengine wao. Na hakika Akhera ni yenye daraja kubwa zaidi na fadhila kubwa zaidi.
22Usimfanye mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu, ukaja ukawa wa kulaumiwa uliyetupika.
23Na Mola wako Mlezi ameamrisha kuwa msimuabudu yeyote ila Yeye tu, na wazazi wawili muwatendee wema. Mmoja wao akifikia uzee, naye yuko pamoja nawe, au wote wawili, basi usiwaambie hata, "Ah!" Wala usiwakemee. Na uwaambie maneno ya heshima.
24Na uwainamishie bawa la unyenyekevu kwa kuwaonea rehema. Na useme: Mola wangu Mlezi! Warehemu kama walivyonilea utotoni.
25Mola wenu Mlezi anajua kabisa yaliyo nyoyoni mwenu. Ikiwa nyinyi mtakuwa wema, basi hakika Yeye ni Mwenye kuwaghufiria wanaorudi sana kwake.
26Na mpe aliye jamaa yako haki yake, na masikini, na msafiri; wala usitumie ovyo kwa fujo.
27Hakika watumiao ovyo kwa fujo ni ndugu wa Mashetani. Na Shetani ni mwenye kumkufuru mno Mola wake Mlezi.
28Na ikiwa utawapa mgongo sawasawa, nawe unatafuta rehema kutoka kwa Mola wako Mlezi unayoitaraji, basi sema nao maneno laini.
29Wala usiufanye mkono wako kama uliofungwa shingoni mwako, wala usiukunjue wote kabisa, ukabaki ukilaumiwa uliyefilisika.
30Hakika Mola wako Mlezi humkunjulia riziki amtakaye, na humpimia amtakaye. Hakika Yeye kwa waja wake ni Mwenye kuwajua na kuwaona vyema.
31Wala msiwaue wana wenu kwa kuogopa umasikini. Sisi tunawaruzuku wao na nyinyi. Hakika kuwaua hao kulikuwa ni kosa kubwa.
32Wala msikaribie uzinzi. Hakika huo ni uchafu na njia mbaya.
33Wala msiuwe nafsi ambayo Mwenyezi Mungu amekataza isipokuwa kwa haki. Na aliyeuliwa kwa kudhulumiwa, basi hakika tumempa msimamizi wake mamlaka. Lakini asipitilize kiasi katika kuua. Kwani yeye anasaidiwa.
34Wala msiyakaribie mali ya yatima, isipokuwa kwa njia iliyo nzuri zaidi, mpaka afike utu uzimani. Na timizeni ahadi. Kwa hakika ahadi itaulizwa.
35Na timizeni kipimo mnapopima. Na pimeni kwa mizani zilizo sawa. Hayo ni heri na yenye mwisho bora.
36Wala usiyafuate usiyo na elimu nayo. Hakika kusikia, na kuona, na (ufahamu wa) moyo hivyo vyote itaulizwa juu yake.
37Wala usitembee katika ardhi kwa kiburi. Hakika wewe huwezi kuipasua ardhi na kamwe huwezi kufikia urefu wa milima.
38Hayo yote ubaya wake ni wenye kuchukiza kwa Mola wako Mlezi.
39Hayo ni katika hekima alizokufunulia Mola wako Mlezi. Wala usimweke pamoja na Mwenyezi Mungu mungu mwengine, ukaja ukatupwa katika Jahannamu ukilaumiwa na kufurushwa.
40Je, Mola wenu Mlezi amewateulia nyinyi wavulana, na Yeye akawafanya Malaika ni banati zake? Kwa hakika nyinyi mnasema kauli kubwa.
41Na tumekwishabainisha katika Qur'ani hii ili wapate kukumbuka. Lakini haikuwazidisha ila kuwa mbali nayo.
42Sema: Lau kuwa wangelikuwa pamoja naye miungu mingine kama wasemavyo, basi wangelitafuta njia ya kumfikia Mwenye Kiti cha Enzi.
43Subhanahu Wa Taa'la, (Ametakasika na Ametukuka mbali) kabisa na hayo wanayoyasema.
44Zinamtakasa mbingu zote saba na ardhi na vyote vilivyo ndani yake. Na hakuna kitu ila kinamtakasa kwa sifa zake. Lakini nyinyi hamfahamu kutakasa kwake. Hakika Yeye ni Mpole na Mwenye maghfira.
45Na unaposoma Qur-ani, tunaweka baina yako na wale wasioiamini Akhera pazia linalowafunika.
46Na tunaweka vifuniko juu ya nyoyo zao wasije wakaifahamu, na tunaweka kwenye masikio yao uziwi. Na unapomtaja katika Qur-ani Mola wako Mlezi peke yake, basi wao hugeuka nyuma wakaenda zao.
47Sisi tunajua vyema kabisa sababu wanayosikilizia wanapokusikiliza, na wanaponong'ona. Wanaposema hao madhalimu: Nyinyi hamumfuati isipokuwa mwanamume aliyerogwa.
48Tazama jinsi walivyokupigia mifano. Basi wakapotea. Kwa hivyo hawawezi kuipata njia.
49Na walisema: Je! Tutakapokuwa mifupa na mapande yaliyovurugika, tutafufuliwa kwa umbo jipya?
50Sema: Kuweni hata mawe au chuma.
51Au umbo lolote mnaloliona kubwa katika vifua vyenu. Watasema: Ni nani atakayeturudisha tena? Sema: Yule yule aliyewaumba mara ya kwanza! Watakutikisia vichwa vyao, na watasema: Ni lini hayo? Sema: Labda huenda itakuwa hivi karibuni!
52Siku atakapowaita, nanyi mtamuitikia kwa kumsifu, na mtadhani kuwa hamkukaa isipokuwa muda mdogo tu.
53Waambie waja wangu waseme maneno mazuri, kwa maana hakika Shetani huchochea ugomvi baina yao. Hakika Shetani ni adui aliye dhahiri kwa mwanadamu.
54Mola wenu Mlezi anawajua vilivyo. Akitaka, atawarehemu, na akitaka, atawaadhibu. Na hatukukutuma ili uwe msimamizi wao.
55Na Mola wako Mlezi anawajua vilivyo waliomo mbinguni na katika ardhi. Na hakika tumewafadhilisha baadhi ya Manabii kuliko wengine, na Daudi tulimpa Zaburi.
56Sema: Waombeni hao mnaowadai badala yake Yeye. Hawawezi kuwaondolea madhara, wala kuyaweka pengine.
57Hao ambao wao wanawaomba, wao wenyewe wanatafuta njia ya kwendea kwa Mola wao Mlezi hata miongoni mwao walio karibu mno, na wanataraji rehema zake, na wanaihofu adhabu yake. Hakika adhabu ya Mola wako Mlezi yafaa kutahadhariwa.
58Na hakuna mji wowote ila Sisi tutauteketeza kabla ya Siku ya Kiyama, au tutaupa adhabu kali. Haya yamekwishaandikwa katika Kitabu.
59Na hakuna kinachotuzuia kutuma miujiza ila ni kuwa watu wa zamani waliikanusha. Na tuliwapa Wathamudi ngamia jike kuwa ni Ishara iliyo dhaahiri, lakini walidhulumu kwaye. Nasi hatutumii Ishara isipokuwa kwa ajili ya kuhofisha.
60Na tulipokwambia: Hakika Mola wako Mlezi amekwishawazingira hao watu. Na hatukuifanya ndoto tuliyokuonyesha isipokuwa ni kuwajaribu watu, na mti uliolaaniwa katika Qur-ani. Na tunawahofisha, lakini haiwazidishii isipokuwa uasi mkubwa.
61Na pale tulipowaambia Malaika, "Msujudieni Adam." Wakamsujudia isipokuwa Iblisi. Akasema, "Je, nimsujudie uliyemuumba kwa udongo?"
62Akasema, "Hebu unamuona huyu uliyemtukuza zaidi yangu, ukiniahirisha mpaka Siku ya Kiyama, hapana shaka nitakiangamiza kizazi chake isipokuwa wachache tu."
63Akasema Mwenyezi Mungu: Nenda! Na atakayekufuata katika wao, basi hakika Jahannamu itakuwa ndiyo malipo yenu, malipo yaliyo mengi.
64Na wachochee uwawezao katika wao kwa sauti yako, na wakusanyie jeshi lako la wapandao farasi na waendao kwa miguu. Na shirikiana nao katika mali na wana, na waahidi. Na Shetani hawapi ahadi isipokuwa ya udanganyifu.
65Hakika wewe huna mamlaka yoyote juu ya waja wangu. Na Mola wako Mlezi anatosha kuwa ni Mtegemewa.
66Mola wenu Mlezi ndiye anayewaendeshea merikebu katika bahari ili mtafute katika fadhila zake. Hakika Yeye ni Mwingi wa kukurehemuni.
67Na inapowakuta taabu katika bahari, hao mnaowaomba wanapotea, isipokuwa Yeye tu. Na anapowaokoa mkafika nchi kavu, mnageuka. Ama mwanadamu ni mwingi wa kukufuru.
68Je, mna amani ya kuwa hatawadidimiza katika upande wowote katika nchi kavu, au kwamba hatawatumia tufani la kokoto? Kisha msipate yeyote wa kumtegemea.
69Au mna amani ya kuwa hatawarudisha humo mara nyingine na akawatumia kimbunga cha upepo akawazamisha kwa mlivyokufuru, na kisha msipate wa kuwanusuru kutokana nasi.
70Na hakika tumewatukuza wanadamu, na tukawabeba katika nchi kavu na baharini, na tukawaruzuku katika vitu vizuri vizuri, na tukawafadhilisha kwa fadhila kubwa kuliko wengi miongoni mwa wale tuliowaumba.
71Siku tutakapoita kila kikundi cha watu kwa mujibu wa wakifuatacho, basi atakayepewa kitabu chake kwa mkono wake wa kulia, basi hao watasoma kitabu chao wala hawatadhulumiwa hata chembe.
72Na yule ambaye ni kipofu hapa, basi atakuwa kipofu Akhera, na atakuwa ndiye mpotovu zaidi wa Njia.
73Na hakika walikaribia kukushawishi uache hayo tuliyokufunulia ili utuzulie mengineyo. Na hapo, ndipo wangelikufanya mwandani.
74Na lau kuwa hatukukuweka imara, ungelikaribia kuwaegemea kidogo.
75Hapo basi bila ya shaka, tungelikuonjesha adhabu maradufu ya uhai, na adhabu maradufu ya kifo. Kisha usingepata yeyote wa kukunusuru kutokana nasi.
76Na walitaka kukukera ili wakutoe nchini. Na hapo, wao wasingelibakia humo isipokuwa kwa muda mchache tu.
77Hiyo ndiyo desturi ya Mitume wetu tuliowatuma kabla yako. Wala hutapata mabadiliko katika desturi yetu.
78Simamisha Swala jua linapopinduka mpaka giza la usiku, na Qur-ani ya alfajiri. Hakika Qur-ani ya alfajiri inashuhudiwa daima.
79Na amka usiku kwa ajili ya kufanya ibada kwayo, ni ziada ya sunna hasa kwako wewe. Huenda Mola wako Mlezi akakunyanyua cheo kinachosifika.
80Na sema, "Mola wangu Mlezi! Niingize muingizo mwema, na unitoe kutoka kwema. Na unipe nguvu zinazotoka kwako zinisaidie."
81Na sema, "Haki imefika, na batili imetoweka. Hakika batili lazima itoweke!"
82Na tunateremsha katika Qur-ani yale ambayo ni uponyaji na rehema kwa Waumini. Wala hayawazidishii madhalimu isipokuwa hasara.
83Na tunapomneemesha mtu, hugeuka na kujitenga kando. Na yanapomgusa maovu, hukata tamaa.
84Sema, "Kila mmoja anafanya kwa namna yake. Na Mola wenu Mlezi ndiye anayejua zaidi yule aliyeongoka katika njia."
85Na wanakuuliza habari za Roho. Sema, "Roho ni katika mambo ya Mola wangu Mlezi. Nanyi hamkupewa katika elimu isipokuwa kidogo tu."
86Na tungelipenda, tungeliyaondoa yale tuliyokufunulia. Kisha usingelipata mwakilishi wa kukupigania kwetu kwa haya.
87Isipokuwa iwe rehema itokayo kwa Mola wako Mlezi. Hakika fadhila yake kwako ni kubwa.
88Sema: Wangelikusanyika watu na majini ili walete mfano wa Qur-ani hii, basi hawawezi kuleta mfano wake, hata kama watasaidiana wao kwa wao.
89Na hakika tumewaeleza watu katika Qur-ani hii kwa kila mfano. Lakini wengi wa watu wakakataa isipokuwa kukufuru tu.
90Na walisema, "Hatutakuamini mpaka ututimbulie chemichemi katika ardhi hii.
91Au uwe na bustani ya mitende na mizabibu, na utupitishie mito kati yake ikimiminika.
92Au utuangushie mbingu vipande vipande kama ulivyodai, au utuletee Mwenyezi Mungu na Malaika uso kwa uso.
93Au uwe na nyumba iliyopambwa, au upae mbinguni. Wala hatutaamini kupaa kwako huko mpaka ututeremshie kitabu tukisome.ˮ Sema, “Subhana Rabbi (Ametakasika Mola wangu Mlezi)! Kwani mimi ni nani isipokuwa ni mtu tu Mtume?"
94Na hakikuwazuilia watu kuamini ulipowajia uongofu isipokuwa ni kwamba walisema, "Je, Mwenyezi Mungu alimtuma mtu kuwa ni Mtume?"
95Sema, "Ingelikuwa katika ardhi wapo Malaika wanatembea kwa utulivu wao, basi bila ya shaka tungeliwateremshia Malaika kuwa ni Mtume wao."
96Sema, "Mwenyezi Mungu anatosha kuwa Shahidi baina yangu na nyinyi. Hakika Yeye ana habari zote za waja wake na anawaona vyema."
97Na yule ambaye Mwenyezi Mungu anamuongoa, basi huyo ndiye aliyeongoka. Na yule ambaye anampotoa, basi hutawapatia walinzi wowote badala yake. Na tutawakusanya Siku ya Kiyama hali ya kuwa wanakokotwa juu ya nyuso zao, huku ni vipofu, mabubu, na viziwi. Na makazi yao ni Jahannamu. Kila ukifanya kuzimika, tutazidi kuuchochea uwake kwa nguvu.
98Hayo ni malipo yao kwa sababu walizikataa ishara zetu, na wakasema: Hivyo tukishakuwa mifupa na mapande yaliyovurugika tutafufuliwa kwa umbo jipya?
99Kwani hawakuona ya kwamba Mwenyezi Mungu aliyeumba mbingu na ardhi ni Mwenye kuweza kuumba mfano wao? Na Yeye amewawekea muda usio na shaka yoyote. Lakini madhalimu walikataa isipokuwa kukufuru tu.
100Sema, "Lau kuwa nyinyi mnazimiliki hazina za rehema za Mola wangu Mlezi, basi hapana shaka mngelizuia kwa sababu ya kuhofu kuzitumia. Na mtu tangu hapo tabia yake ni mchoyo mno!"
101Na kwa yakini tulimpa Musa ishara tisa zilizo wazi. Basi waulize Wana wa Israili alipowafikia, na Firauni akamwaambia, "Hakika mimi ninakuona wewe Musa umerogwa!"
102Musa akasema, "Wewe unajua bila ya shaka kuwa haya hakuyateremsha isipokuwa Mola Mlezi wa mbingu na ardhi ili kuwa ni ushahidi wa kuonekana. Na hakika mimi bila ya shaka nakuona wewe, Firauni, kuwa utaangamizwa."
103Basi Firauni akataka kuwafukuza katika nchi. Kwa hivyo tukamzamisha majini yeye na wale waliokuwa pamoja naye wote.
104Na tukawaambia baada yake Wana wa Israili, "Kaeni katika nchi. Na itakapokuja ahadi ya Akhera, tutawaleta nyote pamoja."
105Na kwa Haki tuliiteremsha, na kwa Haki iliteremka. Na hatukukutuma isipokuwa uwe mbashiri na mwonyaji.
106Na Qur-ani tumeigawanya sehemu mbalimbali ili uwasomee watu kwa kituo, na tumeiteremsha kidogo kidogo.
107Sema, "Iaminini au msiiamini. Hakika wale waliopewa elimu kabla yake, wanaposomewa hii, huanguka kifudifudi wanasujudu.
108Na wanasema, 'Subhana Rabbina (Ametakasika Mola wetu Mlezi)! Hakika ahadi ya Mola wetu Mlezi lazima itimizwe!'"
109Na huanguka kifudifudi na huku wanalia, na inawazidisha unyenyekevu.
110Sema, "Mwombeni Allah (Mwenyezi Mungu), au mwombeni Ar-Rahman (Mwingi wa rehema), kwa jina lolote mnalomwita. Hakika, Yeye ana majina mazuri zaidi." Wala usiswali Swala yako kwa sauti kubwa sana, wala usiifiche kwa sauti ndogo sana, bali shika njia ya kati na kati ya hizo.
111Na sema: Alhamdulillah (sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu) ambaye hakujifanyia mwana yeyote, wala hana mshirika yeyote katika ufalme, wala hana mlinzi yeyote wa kumsaidia kwa sababu ya udhaifu. Na mtukuze kwa utukufu mkubwa.